• HABARI MPYA

    Sunday, November 05, 2017

    SIMBA, YANGA NA MIAMBA MINGINE ITAKAYOVAANA KOMBE LA MAPINDUZI YATAJWA

    Na Salum Vuai, ZANZIBAR
    SIMBA SC, Yanga SC na Azam FC, ni miongoni mwa timu zitakazoshiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi mwaka 2018.
    Jumla ya timu kumi zimepangwa kutoana jasho kwenye ngarambe hizo, nne ambazo zinatoka Unguja ni JKU, Zimamoto, Taifa ya Jang’ombe na Mlandege huku Shaba SC na wakongwe wa soka visiwani Zanzibar, Jamhuri zikikiwakilisha kisiwa cha Pemba.
    Kamati ya mashindano hayo ambayo leo imekutana na waandishi wa habari, imeeleza kuwa timu moja inatarajiwa kutoka nje ya Tanzania, lakini bado haijajulikana ingawa inatazamwia kutoka Kenya au Uganda.
    Kamati hiyo imesema inaendelea na maandalizi ya michuano hiyo iliyokwishapata umaarufu mkubwa, ambayo mara hii itafanyika wakati Zanzibar ikiadhimisha miaka 54 ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.
    Shughuli hiyo inatarajiwa kuanza rasmi mwishoni mwa mwezi Disemba na mchezo wa fainali utarindima uwanja wa Amaan usiku wa  Januari 13, 2018.
    Kamati ya mashindano hayo inaendelea kuongozwa na Sharifa Khamis Salim (Mwenyekiti), Gulam Abdalla Rashid (Makamu Mwenyekiti) na Khamis Abdalla Said (Katibu).
    Wajumbe ni Issa Mlingoti Ali, Dk. Ally Saleh Mwinyikai,  Ali Khalil Mirza, Khamis Mzee Ali, Ravia Idarous Faina (Rais wa ZFA), Ali Mohammed Ali (Makamu Rais wa ZFA), Mohammed Ali Hilali (Tedy) ambaye ni Katibu Mkuu wa ZFA na Juma Mmanga.
    Azam FC ndiyo wanaoushikilia ubingwa wa michuano huo walioupata baada ya kuichapa Simba SC 1-0, bao lililofungwa na Himid Mao kwa staili ya ‘Mama mkanye mwanao’ kutoka umbali wa takriban mita 40.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA, YANGA NA MIAMBA MINGINE ITAKAYOVAANA KOMBE LA MAPINDUZI YATAJWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top