• HABARI MPYA

    Wednesday, November 01, 2017

    MTIBWA SUGAR WAJIVUNIA REKODI YA KUTOFUNGWA NA NDANDA FC

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MTIBWA Sugar inaondoka kesho Manungu mkoani Morogoro kwenda Mtwara kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya wenyeji, Ndanda FC Jumamosi Uwanja wa Nangwanda Sijaona.
    Lakini katika msafara huo, Mtibwa Sugar haitakuwa na wachezaji wake watatu majeruhi, kipa Shaaban Kado, beki Salum Kanoni na kiungo Haroun Chanongo.
    Katibu Msaidizi wa timu, Abubakar Maswabur amesema kwamba wachezaji hao watatu wanaendelea na matibabu na wanatarajiwa kurejea katikati ya mwezi huu.
    Kikosi cha Mtibwa Sugar kinaondoka kesho Manungu kwenda Mtwara kwa ajili ya mchezo na Ndanda FC 

    Maswabur amesema wanakwenda kwenye mchezo huo wakiwa wanajivunia kutowahi kufungwa na Ndanda popote tangu timu hiyo ya Mtwara ilipopanda Ligi Kuu mwaka 2014.  Katika michezo sita ambayo timu hizo zilikutana, Mtibwa wameshinda mara nne na mingine miwili wametoka sare. Mtibwa Sugar wamefunga jumla ya mabao 10 katika mechi hizo, huku Ndanda wakifunga mabao manne.
    Kwa ujumla, Ligi Kuu itaendelea Ijumaa, Maji Maji FC wakiikaribisha Stand United Uwanja wa Maji Maji mjini Songea, wakati Jumamosi Singida watakuwa wenyeji wa Yanga Uwanja wa Namfua, Singida na Ndanda FC wataikaribisha Mtibwa Sugar Uwanja wa Nangwanda.
    Mechi nyingine za Jumamosi, Kagera Sugar wataikaribisha Tanzania Prisons Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, Njombe Mji FC wataikaribisha Mbao FC Uwanja wa Saba Saba na Azam FC watakuwa wenyeji wa Ruvu Shooting Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Jumapili kutakuwa na mechi mbili, mbali na Mbeya City kuwa wenyeji wa Simba, Lipuli FC nao wataikaribisha Mwadui FC Uwanja wa Samora mjini Iringa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR WAJIVUNIA REKODI YA KUTOFUNGWA NA NDANDA FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top