• HABARI MPYA

    Friday, March 17, 2017

    KCCA WATAMBA KUWAVUA UBINGWA MAMELODI KESHO

    KIPA wa timu ya Mamlaka ya Jiji la Kampala (KCCA), Benjamin Ochan amesema kwamba wana uwezo wa kuwatoa mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.
    Mabingwa hao wa Uganda watakuwa wenyeji wa timu ya Pretoria kesho katika mchezo wa marudiano wa hatua ya 32 Bora Ligi ya Mabingwa Afrika Uwanja wa Philip Omondi. Katika mchezo wa kwanza, Mamelodi Sundowns ilishinda 2-1 mjini Pretoria na maana yake KCCA inaweza kufanikiwa kuangusha mbuyu iwapo itashinda 1-0 kesho.
    “Tuna uwezo wa kuwatoa Sundowns na kuwa sehemu ya historia. Tunafahamu ushindani uliopo mbele yetu, kwa sababu tunakabiliana na mabingwa watetezi, lakini tuna njaa ya kuwa timu ya kwanza ya Uganda kufika hatua ya makundi,”alisema Ochan.
    KCCA imesema kwamba wana uwezo wa kuwatoa mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini

    Mzuia michomo huyo, Ochan atauelekeza ushindi huo kwa marehemu baba yake, Dominic B. Elepu, aliyefariki dunia mapema wiki hii.
    Kwa upande wake, kocha wa KCCA, Mike Mutebi amesema kwamba wachezaji wake wapo tayari kwa mchezo huo.
    “Hali ndani ya kambi iko sawa, lakini muhimu zaidi ni wachezaji wanajiamini wanaweza kuitoa Sundowns. Ninajiamini kwamba tunaweza kupata matokeo tunayoyahitaji, kwa sababu mtindo wetu wa uchezaji unatuhakikishia kutengeneza nafasi na tutazitengeneza. Tunachotakiwa ni kuwa wenye madhara na kuwaweka kambi,”amesema.
    Waganda hao kesho watamtegemea mshambuliaji wao Geoffrey Sserunkuma ambaye amefunga mabao matatu katika kila mechi kati ya tatu zilizopita za Ligi ya Mabingwa na anataka kuendelea kufunga. 
    Wakati huo huo; Kocha wa Mamelodi Sundowns, Pitso Mosimane ambaye alilalamikia umaliziaji mbovu wa timu yake katika mchezo wa kwanza, amesema anatarajia mechi ngumu dhidi ya wenyeji wao, .
    "Kuongoza kwa mabao 2-1 ni kipaumbele, lakini pia si kipaumbele. Ni kipaumbele kama hatutaruhusu bao au tutapata sare; lakini kama wakifunga si kipaumbele, utakuwa mchezo wa wazi. Ni mchezo wa yeyote,” amesema Mosimane.
    MECHI ZA WIKIENDI HII LIGI YA MABINGWA
    Jumamosi Machi 18, 2017
    KCCA (Uganda) vs Mamelodi Sundowns (Afrika Kusini) (1-2)
    RC Kadiogo (Burkina Faso) vs USM Alger (Algeria) (0-2)
    El Merreikh (Sudan) vs Rivers United (Nigeria) (0-3)
    FUS Rabat (Morocco) vs Ahly Tripoli (Libya) (0-2)
    Mounana (Gabon) vs Wydad Athletic Club (Morocco) (0-1)
    Zanaco (Zambia) vs Yanga SC (Tanzania) (1-1)
    CNaPs (Madagascar) vs Coton Sport (Cameroon) (0-1)
    Jumapili, Machi 19, 2017
    AS Tanda (Ivory Coast) vs Etoile du Sahel (0-3)
    Horoya (Guinea) vs Esperance (1-3)
    Barrack Young Controllers (Liberia) vs Ferroviario Beira (Msumbiji) (0-2)
    Enugu Rangers (Nigeria) vs Zamalek (Misri) (1-4)
    AS Vita (DRC) vs Ports Authority (Gambia) (1-1)
    Bidvest (Afrika Kusini) vs Al Ahly (Misri) (0-1)
    Caps United (Zimbabwe) vs TP Mazembe (DRC) (1-1)
    Saint George (Ethiopia) vs AC Leopards (Kongo) (1-0)
    Port Louis (Mauritius) vs El Hilal (Sudan) (0-3)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KCCA WATAMBA KUWAVUA UBINGWA MAMELODI KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top