• HABARI MPYA

    Friday, March 17, 2017

    FIFA YAISIMAMISHA MALI BAADA YA SERIKALI KUFUKUZA VIONGOZI

    Na Mwandishi Wetu, ZURICH
    SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa (FIFA) limezifngia timu za Mali kushiriki yote ya kimataifa baada ya Serikali kuingilia uendeshwaji wa shirikisho la soka la nchi hiyo.
    Maana yake Mali haitaendelea na mechi za kufuzu Kombe la Dunia na ilitarajiwa kumenyana na Morocco Agosti 28 na klabu za nchi hiyo zimekwishatolewa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa.
    Hatua hiyo inafuatia Waziri wa Michezo wa Mali, kuwaondoa madarakani viongozi wa Shirikisho la Soka la nchi hiyo (FEMAFOOT).
    Na FIFA imesema inaweza kuondoa adhabu hiyo iwapo tu Serikali ya Mali itabatilisha uamuzi wake dhidi ya Kamati ya Utendaji ya FEMAFOOT na kumrejesha madarakani Rais wake, Boubacar Baba Diarra.
    Mali ilisimamishwa siku moja baada ya uchaguzi wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Ahmad Ahmad wa Madagascar akimshinda Issa Hayatou wa Cameroon aliyedumu kwa miaka 29 madarakani.
    "Uamuzi wa Wizara unakwenda kinyume na uhuru wa vyama vya soka,"imesema taarifa ya FIFA.


    Wizara ya Michezo ya Mali imesema itaendelea kushikilia msimamo wake na haijali adhabu hiyo.
    "Ni uamuzi wa Serikali na hautabadilika," alisema Waziri wa Michezo, Mwanasheria Amadou Diarra Yalcouye na kuongeza; "FIFA haiwezi kuifanya serikali ibadili uamuzi huu. Muda si mrefu Wizara itaaunda Kamati ya Muda ya kuendesha na kuiunganisha familia ya soka,".
    Mali ilivurunda katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2017 nchini Gabon, ikifunga bao moja tu wakifungwa na Ghana na kutoa sare na Misri na Uganda.
    Kwa sasa nchi hiyo inashika nafasi ya 61 katika viwango vya ubora wa soka vya FIFA na namba 12 kwa Afrika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: FIFA YAISIMAMISHA MALI BAADA YA SERIKALI KUFUKUZA VIONGOZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top