• HABARI MPYA

    Tuesday, November 01, 2016

    TAIFA STARS KUIFUATA ZIMBABWE KIRAFIKI HARARE NOVEMBA 13

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BAADA ya kukosa mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Ethiopia, timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ imepata mwaliko wa kucheza na Zimbabwe katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa unaotarajiwa kufanyika jijini Harare, Novemba 13, mwaka huu.
    Kama ilivyotokea kwa Ethiopia kuomba nafasi hiyo kwa Tanzania, pia Zimbabwe imefanya hivyo na mara moja Tanzania imethibitisha kucheza mchezo huo wa kirafiki wa kimataifa wenye kutoa tathmini ubora ili kuingia kwenye viwango vya ubora vya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
    Kuikosa Ethiopia ambayo ilitoa taarifa baadaye kuwa isingeweza kuihodhi Taifa Stars kwa sababu ya hali mbaya ya hewa kwa kipindi cha Oktoba mwanzoni, kulisababisha Tanzania iliyokuwa imejiandaa kucheza mechi hiyo kushushwa kwa kiwango kikubwa nafasi ya ubora wa viwango vya FIFA kutoka ya 132 hadi zaidi ya 144. Zimbambwe kwa sasa ni ya 110 na Ethiopia ni ya 126.
    Tayari Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa amepewa majukumu ya kuanza maandalizi na wakati wowote wiki hii atatangaza kikosi ambacho kitawavaa vijana hao wa Mheshimiwa Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe.
    “Ni kipimo kizuri, ni timu nzuri kucheza nayo,” alisema Mkwasa.
    Taifa Stars ambayo kwa sasa haina mashindano au kujiandaa na mashindano yoyote baada ya kutolewa nafasi ya kuwania Kombe la Mataifa ya Afrika, inajipanga huku ikisubiria ratiba mpya za Baraza la Mpira wa Miguu Afrika Mashariki (CECAFA), Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAIFA STARS KUIFUATA ZIMBABWE KIRAFIKI HARARE NOVEMBA 13 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top