• HABARI MPYA

    Monday, December 21, 2015

    MAJWEGA AFUNGUA AKAUNTI YA MABAO SIMBA SC, LAKINI WAFUNGWA 3-1 NA TIMU YA MATOLA

    Na Mwandishi Wetu, GEITA
    WINGA Mganda, Brian Majwega amefunga bao lake la kwanza Simba SC leo, lakini bahati mbaya Wekundu wa Msimbazi wamelala 3-1 mbele ya timu ya Daraja la Pili, Geita Gold Mine.
    Katika mchezo huo wa kirafiki uliofanyika Uwanja wa shule ya Wajja Spring, Geita, Simba SC ilipata bao lake dakika ya 32 baada ya Majwega kufunga kwa ustadi.
    Hata hivyo, Geita inayofundishwa na Nahodha na Kocha Msaidizi wa zamani wa Simba SC, Suleiman Abdallah Matola ilizinduka na kuanza kufunga mfululizo.
    Brian Majwega amefunga bao lake la kwanza Simba SC leo, lakini bahati mbaya timu imelala 3-1

    Pastory Kaisi aliisawazishia Geita kwa mkwaju wa penati dakika ya 44, baada ya kipa wa Simba Peter Manyika Jr. kumchezea rafu mshambuliaji huyo na Juvenile Pastory akafunga la pili dakika ya 62.
    Kiungo wa zamani wa Yanga SC, Emmanuel Swita akafunga la tatu dakika ya 84 kwa mkwaju wa penalti pia baada ya beki Mrundi, Emery Nimubona kuunawa mpira ndani ya eneo la hatari.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Peter Manyika, Said Issa, Emery Nimubona, Novat Lufunga, Mohammed Fakhi, Awadh Juma, Joseph Kimwaga, Danny Lyanga, Paul Kiongera, Hajji Ugando na Brian Majwega.
    Wachezaji wa Geita Gold Mine wakiwasalimia wachezaji wa Simba SC kabla ya mchezo

    Baada ya mchezo huo, Simba SC imerejea mjini Mwanza kuendelea na maandalizi ya mchezo wake ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mwadui utakaopigwa Jumamosi mjini Shinyanga.
    Ikumbukwe juzi, Simba SC ililazimishwa sare ya 1-1 na Toto Africans katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu Uwanja wa CCM Kirumba. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAJWEGA AFUNGUA AKAUNTI YA MABAO SIMBA SC, LAKINI WAFUNGWA 3-1 NA TIMU YA MATOLA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top