• HABARI MPYA

    Saturday, August 30, 2014

    MASIKINI TEGETE, KUTOKA JERI MABAO HADI JERY MAFYONGO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MWAKA 2006 ndipo jina la Jerson John Tegete lilipoanza kuchomoza katika soka ya Tanzania, kijana mdogo mwenye kipaji cha kufunga mabao kutoka mjini Mwanza.
    Kwa kipaji chake, akahamishiwa sekondari ya Makongo, Dar es Salaam ili kuendelezwa zaidi kisoka na mwaka 2007 akiwa hajaanza hata kucheza klabu ya Daraja la Kwanza, akachukuliwa timu ya taifa.
    Kocha Mbrazil, Marcio Maximo alimchukua kijana huyo akiwa mdogo mno ili kumkomaza katika kikosi chake, kwa matumaini baadaye aje kuwa tegemeo la mabao la Taifa Stars. Tegete alikuwa havai hata jezi kwenye mechi za Stars, lakini Maximo alikwenda naye kwenye kambi ya mwezi mmoja Brazil na baadaye nchi za Scandinavia.
    Nini tatizo? Jerry Tegete baada ya kukosa bao la wazi dhidi ya KMKM Jumatano usiku
    Ana Mapepo? Haruna Niyonzima akimtuliza kichwa Tegete, huku Mrisho Ngassa akicheka nyuma yao

    Mwaka 2008, Tegete akasajiliwa na klabu ya Yanga SC na kufika mwaka 2008, mtoto huyo wa kocha maarufu mjini Mwanza, John Tegete akaanza kucheza na kung’ara.
    Mabao ya Tegete yaliisaidia Tanzania kukata tiketi ya kucheza michuano ya kwanza ya CHAN mwaka 2009 nchini Ivory Coast. 
    Tegete akawa tegemeo kubwa la Yanga SC kufunga mabao katika mechi dhidi ya watani wa jadi na alikuwa, Simba SC akimgaragaza sana Juma Kaseja kwenye viwanja tofauti.
    Mara ya mwisho Tegete kufunga dhidi ya Simba SC, ilikuwa Oktoba 16, mwaka 2010 Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza akimtungua Kaseja dakika ya 70, Yanga SC ikishinda 1-0.
    Na tangu amefunga bao hilo Kirumba, Tegete akaanza kupoteza makali yake taratibu hadi kufika misimu miwili iliyopita umaarufu wake wa kucheka na nyavu umetoweka kabisa.
    Anafunga mara chache, lakini kwa sasa si tegemeo tena la mabao Yanga SC hata katika michezo ya kirafiki.
    Katika mchezo wa kirafiki dhidi ya KMKM Uwanja wa Amaan Zanzibar wiki hii, Tegete alikosa mabao mawili ambayo ni vigumu kwa mtu yeyote kuamini kama Tegete yule aliyeitwa ‘Jerry Mabao’ anapiga mafyongo namna ile.
    Simon Msuva alipangua mabeki wa KMKM akaingia hadi kwenye sita, akiwa anatazama na kipa akampasia Tegete aliyekuwa anatazamana na nyavu- huwezi amini jamaa alipiga juu.
    Kwa hasira za kukosa mabao akapiga ngumi chini na kusikitika sana, akiwa yeye mwenyewe haamini macho yake juu ya mazingira ambayo alikosa bao. 
    Tegete akapata nafasi nyingine nzuri, alipewa mpira akiwa nje kidogo ya sita anatazama na kipa, akapiga fyongo na hapo hapo kocha Maximo akamuita benchi na nafasi yake kuchukuliwa na Said Bahanuzi.
    Tegete akifumua shuti nje kidogo ya sita, lakini akakosa bao
    Tegete akiwa haamini macho yake baada ya kukosa bao la wazi

    Alipofika kwenye benchi, wachezaji rafiki zake, Mrisho Ngassa na Haruna Niyonzima wakampokea na kuanza kumtania kwamba anahitaji kuaguliwa. Niyonzima alishika kichwa cha Tegete na kuanza kukitikisa mithili ya mtu anayemtuliza mtu mwenye mapepo.
    Walikuwa wanafanya kama mzaha, lakini ukweli ni kwamba ni hali ambayo inasikitisha sana juu ya Tegete. Huu ndiyo ulikuwa wakati wa Tegete kuibeba nchi na klabu yake, baada ya uwekezaji mkubwa uliofanyika kwake.
    Lakini ni nini kimemsibu hata amepoteza makali yake uwanjani? Ni zile sifa alizokuwa akipata wakati anafanya vizuri zilimfanya akabweteka na kupotea kwenye mstari? Au ni tatizo gani linalomsumbua Tegete hivi sasa hata akili yake haipo uwanjani tena?
    Yuko fiti kimwili, kwa sababu wakati wote anafanya mazoezi na wenzake, lakini anapokuwa uwanjani huwezi kuelewa anafanya nini- nini kinamsumbua Tegete?
    Ana kipaji. Sahihi kabisa. Bado ana uwezo. Ndiyo. Lakini ana matatizo kwa sasa. Je, anasaidiwaje? Nani rafiki yake, akina nani watu wake wa karibu kwa sasa. Wanamshauri nini wakati huu, kwenda kwa waganga kuloga zaidi au kutuliza akili yake aweze kucheza mpira vizuri.
    Viongozi wa klabu yake nao wanawajibika vipi kukinusuru kipaji chake, au wanasubiri apotee kabisa ndipo wamtupie virago? Tegete hayuko vizuri kwa sasa, lakini bado ana uwezo, Yanga wakae naye wairudishe akili yake uwanjani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MASIKINI TEGETE, KUTOKA JERI MABAO HADI JERY MAFYONGO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top