• HABARI MPYA

    Sunday, June 22, 2014

    KAZI IMEANZA, SIMBA SC YASAINI BEKI LA TAIFA STARS MIAKA MITATU...YANGA NA MAGAZETI YAO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KAZI imeanza. Simba SC imesajili mchezaji wa kwanza kabisa kwa ajili ya msimu ujao, ambaye ni chipukizi wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars Joram Nason Mgeveke.
    Mchezaji huyo chipukizi pekee kutoka kikosi cha maboresho aliyebaki Taifa Stars chini ya kocha Mholanzi Mart Nooij, amesaini Mkataba wa miaka mitatu leo.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, Joram amesaini mjini Iringa na rasmi sasa ni mchezaji wa Simba SC.
    Kifaa cha kwanza 2014-2015; Joram Mgeveke akipeana mikono na Hans Poppe baada ya kusiani Mkataba wa miaka mitatu na Simba SC. Chini anasaini.


    “Tuna muda mfupi sana kwa ajili ya kufanya usajili, sasa tuna orodha ya wachezaji waliopendekezwa, kwa hiyo tunaanza kuwapandia ndege kuwafuata na kumalizana nao, ndani na nje ya nchi. Tumeanza na Joram, kwa sababu yuko Taifa Stars ambayo inakwenda kambini Botswana,”alisema Poppe.   
    Poppe amewahakikishia wana Simba SC kwamba safari hii watasajili wachezaji bora ambao watarejesha heshima ya klabu hiyo msimu ujao.
    Kwa upande wake, beki huyo mwenye misuli anayecheza nafasi za kati za ulinzi, amesema kwamba amefurahi mno kujiunga na Simba SC kwa sababu ni timu kubwa, ambayo anaamini itainua kiwango chake na kumfungulia milango zaidi ya mafanikio.
    Joram Mgeveke wa pili kutoka kushoto waliosimama akiwa kikosini Stars dhidi ya Malawi

    “Kwa kweli nimefurahi sana kujiunga na Simba SC, ni timu kubwa na ya kihistoria hapa Tanzania ambayo wamepita wachezaji wengi wazuri, ambao na mimi ningependea kufuata nyayo zao,”amesema.
    Beki huyo alicheza kwa dakika 75 mechi ya kirafiki ya Tanzania na Malawi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambayo bao pekee la Amri Kiemba wa Simba SC liliipa Taifa Stars ushindi wa 1-0 kabla ya kumpisha Kevin Yondan wa Yanga.
    Tangu hapo amekuwemo kwenye orodha ya wachezaji 18 walioshiriki mechi zote za Stars dhidi ya Zimbabwe kufuzu Mataifa ya Afrika kama mchezaji wa akiba.
    Nyota Njema ndiyo iliyomuibua kinda huyo mwenye umri wa miaka 22, baadaye akachezea Polisi na Lipuli zote za Iringa, kabla ya kuchukuliwa timu ya mkoa, ambayo ilimfungulia milango ya kuingia Taifa Stars kupitia mpango wa maboresho. Katibu wa Lipuli, Willy Chikweo ametoa baraka zake zote juu ya usajili huo. “Kuanzia sasa, Joram ni wa Simba SC, kwa roho safi kabisa na tunamtakia kila la heri,”amesema katibu huyo.
    Wakati Simba SC inafanikisha usajili wa mchezaji wa kwanza wa msimu ujao, watani wa jadi Yanga SC wanaendelea kupamba kurasa za magazeti kwa majina ya wachezaji tofauti ambao inadaiwa wanataka kuwasajili kutoka sehemu mbalimbali duniani.
    Na wakati dirisha la usajili linafungwa mwishoni mwa mwezi huu, hakuna mchezaji hata mmoja ambaye hadi asa Yanga SC imesema rasmi imemsainisha Mkataba, huku ikiwa tayari imewapoteza Frank Domayo na Mrundi Didier Kavumbangu waliohamia Azam FC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAZI IMEANZA, SIMBA SC YASAINI BEKI LA TAIFA STARS MIAKA MITATU...YANGA NA MAGAZETI YAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top