• HABARI MPYA

    Monday, March 09, 2020

    MECHI YA WATANI YAINGIZA SH. MILIONI 545 YANGA IKIICHAPA SIMBA 1-0 BAO PEKEE LA MORRISON

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MECHI ya watani wa jadi, Yanga na Simba jana Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam imeingiza kiasi Sh. 545, 422,000 kutokana na watazamaji 59,325 waliolipa viingilio. 
    Kiasi hicho ni ongezeko kutoka mapato ya mechi ya kwanza Januari 4, mwaka huu ambayo iliingiza Sh. Milioni 539 kutokana na watazamaji wapatao 57,000 timu hizo zikitoka sare ya 2-2.
    Shujaa wa Yanga SC jana alikuwa kiungo mshambuliaji Mghana, Bernard Morrison aliyefunga bao hilo pekee la ushindi dakika ya 44 kwa shuti la mpira wa adhabu kutoka umbali wa mita 25.
    Morrison, mchezaji wa zamani wa Heart of Lions, Ashanti Gold za kwao Ghana, AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Delhi Dynamos FC ya India na Orlando Pirates ya Afrika Kusini alifunga bao hilo baada ya yeye mwenyewe kuchezewa rafu na kungo Jonas Gerlad Mkude. 
    Mchezo wa jana ulihudhuriwa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Rais wa Shrikisho la Soka Tanzania (TFF), Ahmad Ahmad na Wenyekiti wa klabu zote, Dk. Mshindo Msolla wa Yanga na Mohamed ‘Mo’ Dewji wa Simba.   
    Yanga imeafikisha pointi 50 baada ya ushindi wa jana katika mchezo wa 25 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya tatu, sasa ikizidiwa pointi moja Azam FC inayoshika nafasi ya pili ingawa mecheza mechi mbili zaidi.
    Mabingwa watetezi, Simba SC wanaendelea kuongoza Ligi Kuu kwa mbali, wakiwa na pointi 68 baada ya kucheza mechi 27.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MECHI YA WATANI YAINGIZA SH. MILIONI 545 YANGA IKIICHAPA SIMBA 1-0 BAO PEKEE LA MORRISON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top