• HABARI MPYA

    Saturday, December 22, 2018

    WAZIRI KAKUNDA MGENI RASMI MECHI YA SIMBA SC NA NKANA FC KESHO UWANJA WA TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WAZIRI wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Joseph Kakunda atakuwa mgeni rasmi katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Nkana FC utakaopigwa kesho kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
    Simba SC watakuwa wenyeji wa Nkana FC kesho kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa Taifa wakihitaji ushindi wa 1-0 ili kuingia hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kufungwa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza Jumapili iliyopita mjini Kitwe, Zambia.
    Mara ya mwisho Tanzania kuingiza timu hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ilikuwa mwaka 2003 na walikuwa Simba SC ndiyo waliofika hatua hiyo, wakifuata nyayo za wapinzani wao wa jadi, Yanga SC waliokuwa timu ya kwanza kufikia mafanikio hayo mwaka 1998.

    Kocha Mbelgiji wa Simba SC, Patrick J Aussems anaamini kikosi chake kitapinfua matokeo kesho na kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa.
    Mchezo wa kesho utachezeshwa na marefa kutoka nchi jirani, Kenya ambao ni Peter Waweru atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera Gilbert Cheruiyot na Tony Kidiya.
    Simba SC ndiyo timu pekee ya Tanzania iliyobaki kwenye michuano ya Afrika baada ya kutolewa kwa Mtibwa Sugar katika Kombe la Shirikisho la Soka Afrika kwa vipigo vya nyumbani na ugenini baada ya jana kuchapwa 2-1 na KCCA ya Uganda Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam.
    Kwa kipigo hicho, Mtibwa Sugar imetupwa nje kwa jumla ya mabao 5-1, baada uya kuchapwa 3-0 kwenye mchezo wa kwanza wiki iliyopita mjini Kampala, Uganda.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAZIRI KAKUNDA MGENI RASMI MECHI YA SIMBA SC NA NKANA FC KESHO UWANJA WA TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top