• HABARI MPYA

    Monday, December 24, 2018

    TAMBWE APIGA HAT-TRICK YANGA YAICHAPA TUKUYU 4-0 NA KUSONGA MBELE ASFC

    Na Sada Salmin, DAR ES SALAAM
    VIGOGO, Yanga SC wamefanikiwa kuingia hatua ya 32 Bora michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation (ASFC) baada ya ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Tukuyu Stars ya Mbeya jioni ya leo Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Ushindi wa leo wa Yanga umetokana na mabao ya wachezaji wake wa kigeni, Mrundi Amissi Joselyn Tambwe aliyefunga matatu dakika za 14, 36 na 55 na Heritier Makambo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) dakika ya 80.
    Mchezaji mpya, kiungo mkongwe Haruna Moshi Shaaban ‘Boban’ alianzishwa leo, lakini akawa na mwanzo mbaya baada ya kuumia dakika ya 24 tu na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Deus Kaseke.  
    Mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe akishangilia baada ya kufunga mabao matatu katika ushindi wa 4-0 dhidi ya Tukuyu Stars
    Kiungo wa Yanga SC, Mrisho Ngassa akimtoka mchezaji wa Tukuyu Stars leo 
    Mshambuliaji wa Yanga, Heritier Makambo akimtoka beki wa Tukuyu Stars
    Kiungo wa Yanga, Ibrahim Ajibu akimtoka beki wa Tukuyu Stars, Richard Businge
    Haruna Moshi 'Boban' akitolewa nje baada ya kuumia mapema tu kipindi cha kwanza
    Amissi Tambwe baada ya kukabidhiwa mpira wake leo
    Kikosi cha Yanga SC kilichoanza katika mchezo wa leo Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam


    Kikosi cha Tukuyu Stars kilichoanza katika mchezo wa leo Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam

    Kipa Mkongo, Klaus Kindoki alianzishwa tena leo na akadaka kwa umakini mkubwa bila kuruhusu nyavu zake kuguswa. 
    Mechi nyingine za leo Pamba SC ya Jijini Mwanza imewachapa wenyeji Mtwivila City mabao 4-1 Uwanja wa Samora mjini Iringa na na kuungana na Yanga pamoja na timu nyingine 27 kwenda hatua ya 32 Bora.
    Timu nyingine zilizosonga mbele ni JKT Tanzania, Biashara United, Mbeya City, Azam FC, Mbeya Kwanza, Kitayosce, Dodoma FC, Dar City, Lipuli FC, Singida United, Trans Camp, Pan African, Kagera Sugar, Friends Rangers, Rhino Rangers, Namungo FC, Reha FC, Majimaji FC, Boma FC, Cosmopolitan, Polisi Tanzania, KMC, La Familia, Coastal Union, Mighty Elephant na Alliance FC.
    Michuano hiyo itaendelea kesho kwa mechi moja kati ya Stand United na Ashanti United Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga kuanzia Saa 10:00 jioni na hatua ya 64 Bora itakamilishwa Jumatano kwa mechi mbili, Mtibwa Sugar na Kiluvya United Uwanja wa Manungu, Turinia mkoani Morogoro na Simba SC dhidi ya Mashujaa Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Klaus Kindoki, Paul Godfrey, Gardiel Michael, Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Kelvin Yondan/Cleophas Sospeter dk77, Feisal Salum, Pius Buswita, Haruna Moshi/Deus Kaseke dk24, Heritier Makambo, Amissi Tambwe/Mrisho Ngassa dk70 na Ibrahim Ajibu.
    Tukuyu Stars; New Africa, Richard Businge, Julius Leonard, Stanley Ambonisye, Daniel Evans, Elisha Godrick/Gasper Samuel dk70, Maluwe Omar, Richard Amon, Monti Stephano/Benjamin Dominick dk34, Lawama Mabena/Baraka Abroad dk67 na Mussa Bomanus.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAMBWE APIGA HAT-TRICK YANGA YAICHAPA TUKUYU 4-0 NA KUSONGA MBELE ASFC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top