• HABARI MPYA

    Sunday, March 05, 2017

    HATA DONALD NGOMA LEO ANAIDHARAU YANGA!

    YANGA SC imeachana na Mkurugenzi wake wa Ufundi, Mholanzi Hans van der Pluijm kwa sababu ya hali mbaya ya kifedha inayoikabili klabu hiyo kwa sasa.
    Wazi Yanga imeingia katika hali ngumu kufuatia misukosuko ya Mwenyekiti wake, Yussuf Manji ambaye inadaiwa akaunti zake zimefungwa kufuatia matatizo yake na Serikali.
    Manji yupo katika wakati mgumu kwa sasa na Yanga iliyokuwa inamtegemea kwa kila kitu kama Mwenyekiti na mfadhili inajikuta katika wakati mgumu pia.
    Ikumbukwe Manji aliingia Yanga mwaka 2006 kama mfadhili kupitia kampuni yake ya Loto Kitita, wakati huo Mwenyekiti wa klabu alikuwa Francis Kifukwe.
    Tangu hapo Manji akajipa majukumu zaidi ya kuisaidia Yanga kiasi cha kuzidi kuwa mtu muhimu na tegemeo la klabu kifedha.
    Tangu hapo akashuhudia Yanga ikiongozwa na Wenyeviti wawili zaidi, wote Mawakili, Imani Mahugila Madega na Lloyd Baharagu Nchunga kabla ya mwaka 2012 kuwa Mwenyekiti yeye mwenyewe.
    Wakati fulani Yanga ikapata udhamini wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) uliodumu kwa takriban miaka 10 waliomsaidia sana Manji kuisaidia kifedha klabu hiyo.
    Pamoja na mgogoro uliojitokeza mwaka jana hadi Yanga kuachana na TBL, lakini tayari kampuni hiyo ya bia ilikwishapanga kuacha kuidhamini klabu hiyo na mahasimu wao, Simba na ndiyo maana hata zile mechi za Nani Mtani Jembe zilikufa.
    Manji amekuwa kitu pekee Yanga wanategemea kupata fedha ukiondoa mapato ya milangoni ya mechi zao – na kwa sasa anakabiliwa na wakati mgumu, hivyo klabu nayo inakabiliwa na wakati mgumu pia.
    Mbali na kuamua kuachana na Pluijm, lakini baadhi ya wachezaji wa kigeni wako mbioni kuondoka kutokana na sababu za kimaslahi, miongoni mwao ni beki Mtogo, Vincent Bossou na mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Ngoma.
    Kwa ujumla Yanga ipo katika kipindi kigumu na kama si uzoefu wa Katibu wa sasa, Charles Boniface Mkwasa klabu ingeyumba zaidi.
    Mkwasa amekuwa Yanga kama mchezaji, baadaye kocha na sasa kiongozi, hivyo anaijua vyema klabu na njia za kipitia kuifanya iende. Na siku zinaenda na Yanga haijakwama. 
    Pamoja na hayo, kwa hali ambayo inaikabili klabu hii leo wa kulaumiwa ni wana Yanga wenyewe kujiruhusu klabu imtegemee mtu mmoja.
    Lakini kama klabu ingekuwa na vyanzo vingine vya mapato kama wadhamini na vitegauchumi isingeyumba kiasi kinachozungumzwa leo.
    Kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi wiki hii mchezaji ameusemea ovyo uongozi wa Yanga.
    Huyo ni Donald Ngoma ambaye amesema anataka kuondoka katika timu kutokana na mambo ya ovyo ya uongozi.
    Huwezi kujiuliza Ngoma kwa nini anaidharau Yanga wakati anajua wale viongozi hawana lolote na hawawezi lolote bila Manji.
    Jana nimesoma mtu mmoja ameandika kama Yanga ingekuwa imekodishwa kwa Yanga Yetu, isingeyumba.
    Manji alitaka kuikodisha Yanga kwa miaka 10 kupitia kampuni yake aliyoianzisha ya Yanga Yetu, lakini hilo likakwama kutokana na baadhi ya wanachama kwenda mahakamani kupinga.  
    Najiuliza, Yanga Yetu ingeweza vipi kuiendesha Yanga ikiwa akaunti zote za Manji zimefungwa na hadi makampuni yake ameyafunga?
    Naona Yanga ingeyumba zaidi kama kungekuwa na karatasi zilizosainiwa kuikabidhi kwa Yanga Yetu kwa miaka 10.
    Hao wanaoisaidia Yanga kwa sasa ni kwa sababu ni mali ya klabu. Wanaojichangisha fedha kwa sasa kuisaidia Yanga kwa sababu wanajua ni mali ya klabu.
    Wakati huu ambao wana Yanga wanapaswa kuungana kumuombea Mwenyekiti wao aondoke katika mtego alionasa na kuwa huru tena ni vyema pia wakatafakari upya mustakabali wa klabu yao.
    Yanga haiwezi tena kurudi kuishi kama ilivyoishi kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita ikimtegemea mtu mmoja.
    Yanga inapaswa kujimudu yenyewe kama klabu kwanza na ili wakitokea watu wengine kama Manji wa kuja kuisaidia, basi wachangie ustawi wa klabu tu.
    Leo hata mtoto mdogo kama Donald Ngoma anaidharau Yanga? Wajitafakari upya.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HATA DONALD NGOMA LEO ANAIDHARAU YANGA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top