• HABARI MPYA

    Monday, September 21, 2015

    HAMISI KIIZA ‘DIEGO’ SASA ‘AWANYIMA USINGIZI’ YANGA SC…NA ANA HASIRA NAO KINOMA!

    Hamisi Friday Kiiza 'Diego' sasa anawanyima usingizi Yanga SC
    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    HAT TRICK ya kwanza ya msimu ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara imetoka kwa mshambuliaji Mganda, Hamisi Friday Kiiza maarufu kama Diego.
    Kiiza alifunga mabao matatu jana Simba SC ikishinda 3-1 dhidi ya timu ngumu, Kagera Sugar ya Bukoba Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Na sasa Simba SC inakwenda kambini Zanzibar kujiandaa na mchezo dhidi ya mahasimu wao, Yanga SC wikiendi hii hapo hapo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Tangu jana mashabiki wa Yanga SC wameanza kumuhofia Kiiza baada ya kuona na kusikia habari zake dhidi ya Kagera Sugar, hususan wakikumbuka alikuwa mchezaji wao.
    Kiiza aliichezea Yanga SC kwa miaka minne kabla ya kutemwa mwaka jana na kocha Mbrazil, Marcio Maximo ambaye alifukuzwa mwaka huo huo, nafasi yake ikichukuliwa na Mholanzi, Hans van der Pluijm.
    Mashabiki wa Yanga SC hawakuridhishwa na kitendo cha kuachwa kwa Kiiza, lakini waliamua kukubali yaishe na mchezaji huyo akarejea kwao Uganda kupumzika.
    Baada ya takriban nusu msimu wa kutokuwa na timu, Kiiza ameibukia kwa mahasimu Simba SC ambao walimsajili baada ya kumuuza mshambuliaji wao mwingine Mganda, Emmanuel Okwi.
    Kiiza alikuwa kipenzi cha mabosi wa Jangwani, hapa anazungumza Abdallah Bin Kleb

    Mwanzoni wakati anaanza kuonekana na jezi ya SImba SC alionekana kama aliyeishiwa hivi, lakini sasa amegeuka kuwa tegemeo la mabao la Wekundu Msimbazi.
    Kiiza amefunga katika mechi, Simba SC ikishinda 1-0 dhidi ya African Sports, 2-0 dhidi ya Mgambo JKT balo lingine akifunga kiungo Mzimbabwe Justuce Majabvi na jana yote matatu katika ushindi wa 3-0 dhidi ya Kagera.
    Kwa ujumla Kiiza ‘Diego wa Kampala’ hadi sasa ameichezea Simba SC mechi 13, zikiwemo na za kirafiki na kuifungia mabao tisa.  
    Anakwenda katika mechi ya 14 Jumamosi wiki hii dhidi ya timu yake ya zamani, Yanga SC ambayo dhahiri ana hasira nayo baada ya kumtema mwaka jana na atataka kuwadhihirishia walifanya makosa na kukata jina lake katika usajili. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HAMISI KIIZA ‘DIEGO’ SASA ‘AWANYIMA USINGIZI’ YANGA SC…NA ANA HASIRA NAO KINOMA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top