![]() |
| Na Mahmoud Zubeiry |
JANA, rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar
Chillah Tenga alisema kwamba katika sakata la beki wa kimataifa wa Tanzania, Kelvin
Patrick Yondan kudaiwa kusaini mara mbili, lazima kuna klabu moja imefanya
uhuni, maana yake anamtetea beki huyo kwamba hajasaini mara mbili.
Tenga alisema hayo, wakati akijibu swali aliloulizwa kwenye
Mkutano wake na Waandishi wa Habari jana, ofisi za TFF, Ilala mjini Dar es
Salaam, Tenga alisema kwamba kulingana na mfumo wa sasa wa usajili kupitia
mtandao, shirikisho lake halihusiki kabisa na usajili na kwamba hilo ni suala
la mchezaji na klabu.
Tenga alisema anaamini klabu hizo zitamalizana zenyewe
kuhusu mchezaji huyo na akasema suala la Yondan kudaiwa kutoroshwa kambini,
Taifa Stars ili akasaini Yanga halina mantiki kwa sababu mchezaji huyo ni mtu
mzima ana akili zake timamu, ila kinachoendelea kwa sasa ni kelele za kinazi.
Wiki iliyopita, beki Yondan aliibuka anasaini Yanga, kabla
ya klabu yake, Simba aliyoichezea tangu mwaka 2006 kudai bado ina mkataba naye
na wapinzani wao hao wa jadi, wamefanya uhuni kuzungumza naye na kumsajili
wakijua hajamaliza mkataba na klabu yake.
Lakini Yondan mwenyewe alikana kusaini Simba na kusistiza
amesaini Yanga tu, waliompa Sh. Milioni 30 kwa mkataba wa miaka miwili.
Suala la Yondan limeteka hisia za vyombo vingi vya habari nchini
tangu wiki iliyopita.
Mapema wiki iliyopita, BIN ZUBEIRY ilikuwa chombo cha
kwanza cha habari kuufichua mkataba aliosaini Yondana na Yanga na baada ya
kuchapishwa magazetini, Simba SC wakaibuka na kusistiza, mchezaji huyo ana
mkataba na klabu yao.
![]() |
| Yondan kulia akimdhibiti Didier Drogba |
Pia, wakasema Yanga ilikiuka kanuni za usajili kumsajili
mchezaji ambaye bado walikuwa wana mkataba naye na wametishia kuwashitaki FIFA
(Shirikisho la Soka la Kimataifa) wapinzani wao hao.
Lakini awali, Yondan alikaririwa na blog moja (siyo BIN
ZUBEIRY) Aprili mwaka huu akisema hajasaini Yanga bali amesaini Simba.
Lakini uchunguzi uliofanywa na BIN ZUBEIRY ikiwemo kuzungumza na
mchezaji mwenyewe ni kwamba, aliposaini Yanga alipewa fedha nusu na sababu ya
kuwakana ni kuhisi kama hatamaliziwa fedha zake.
Kutokana na hatari ya Yondan kuwageuka, Yanga wakafanya
jitihada za haraka za kummalizia fedha zake Yondan na kumpiga picha akisaini
risiti za malipo yake akiwa ana fedha zake mezani na kukabidhiwa jezi ya
mazoezi.
BIN ZUBEIRY ilikuwa chombo pekee cha habari kupata picha za
Yondan akisaini risiti hizo na kukabidhiwa fedha zake, kabla ya kuvunja kwenye
blogs nyingine na magazeti nchini.
Kwa Yondan kuonekana akisaini risiti hizo, ikawaumiza zaidi
Simba na kutoa tamko rasmi la kulaani kitendo cha wapinzani wao hao wa jadi na
kusema wanapeleka mashitaka FIFA.
Wiki iliyopita Simba waliwasilisha malalamiko yao TFF na Tenga
akawaahidi kulifanyia uchunguzi suala hilo- kwa kuanzia kutaka kujua kama kweli
Yondan aliondoka kambini Taifa Stars kwenda kusaini Yanga kwa kutoroka kambini
au ruhusa.
Tenga amewaahidi Simba, ikibainika Yondan alitoroka kambini
hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa kwa wahusika wote- ingawa maelezo yake ya
jana yanaleta picha tofauti.
Suala la Yondan sasa limekuwa mjadala katika vyombo vya
habari nchini- na tayari hisia za kishabiki katika makala za uchambuzi wa suala
hili zimekwishaanza kujitokeza. Wengi wamekwishaanza kuihukumu Yanga kwamba
imefanya makosa kwa kumsajili Yondan akiwa ana mkataba na Simba.
Kwa uzoefu wangu juu ya masuala kama hili la Yondan- sidhani
kama ipo haja ya kuuhukumu upande wowote kwa sasa, iwe mchezaji au klabu
zenyewe kwa sababu ndio kwanza linaibuka na litakapofika mikononi mwa vyombo
husika naamini mbivu na mbichi zitajulikana.
Yamekwishatokea masuala ya kuumiza kichwa kuhusu mchezaji
kusaini mara mbili- tena wakati huo bado hakuna kanuni madhubuti, lakini
yakapatiwa ufumbuzi, sembuse hili la Yondan linalokuja wakati ambao kanuni za
usajili zimekaa vizuri kabisa.
Hata kama Yondan atakuwa ana mapenzi na Yanga kiasi gani,
ikibainika kweli alikwenda kusaini Yanga wakati bado ana makataba na Simba,
itamgharimu yeye kwanza na Yanga wenyewe.
Nasema kama, kwa sababu namuheshimu Yondan na naheshimu
maelezo yake, akiwa mchezaji mwenye akili zake timamu alisema hajasaini Simba,
amesaini Yanga. Na ninasema kama, pia kwa sababu hizo hizo za kumhesimu
mchezaji huyo na maelezo yake, kwa sababu awali alisema hajasaini Yanga, ameongeza
mkataba na klabu yake Simba.
![]() |
| Yondan anasaini Yanga, akishuhudiwa na mmoja wa wafadhili wa klabu hiyo, Seif Ahmad 'Magari' |
Kuwaita Yanga wahuni kwa sasa ni kuwaonea, kwa sababu hata
TFF imetoa kumbukumbu za hadhi za mchezaji huyo na kusema, mkataba wake na
Simba walionao wao uliisha Mei mwaka huu.
Na ikumbukwe suala la Yondan na Yanga si la jana wala juzi-
mchezaji huyo kwa muda mrefu amekuwa akihusishwa na klabu hiyo ya Jangwani na
hata kwenye klabu yake amekuwa haaminiki wakati mwingine, akidaiwa yeye ni
mnazi wa wapinzani na amekuwa akiwafungisha mabao katika mechi dhidi ya
wapinzani wao.
Mashabiki wenyewe wa Simba wamekuwa hawamkubali mchezaji
huyo linapokuja suala la Yanga- kama ilivyokuwa kwa kiungo na Nahodha wao wa
zamani, Henry Joseph Shindika, ambaye kwa sasa anacheza Norway.
Lakini pia Yondan kufanya mzungumzo na Yanga kwa ajili ya
kuhamia huko, tangu mwaka 2008 enzi hizo klabu hiyo ikiwa chini ya kocha
Msrerbia, Profesa Dusan Savo Kondic, ingawa hawakufanikiwa.
Yanga wamekuwa wakirudi tena na tena kwa Yondan bila
mafanikio. Kwa sababu hiyo, hili si suala la kushitukiza nami bado ninaamini
siku moja beki huyo atacheza Yanga. Sisemi hivyo kwa sababu ya mapenzi yangu na
klabu, bali narejea hukumu ambayo tayari amekwishapewa siku nyingi na mashabiki
wa Simba, kwamba yeye ni Yanga na kwa kuwa wahenga walisema lisemwalo lipo, au
maneno yanaumba- ndio maana ninasema hivyo.
Nimesema ni mapema kumuhukumu Yondan, kwa sababu suala lake
linakuja katika picha ya usajili wa Athumani Iddi ‘Chuji’ kutoka Simba kwenda
Yanga mwaka 2007.
Wakati Yanga ikimsajili Chuji, Simba nayo ilisema mchezaji
huyo bado ana mkataba na klabu yao- lakini mwisho wa siku kijana alicheza
Jangwani.
Watu wanawasilisha hisia zao za hasira katika hili- wakisema
kwamba Yanga imefanya uhuni, lakini wamesahau tabia za wachezaji wa nchi hii?
Unapofika wakati wa usajili wenyewe huhaha huku na kule, bila kuzingatia wana
mikataba na klabu au la.
Pius Kisambale baada ya kukosa kabisa timu mwaka 2009,
aliwahi kunifuata kuniomba nimsaidie kupata timu, nikaenda kumuombea kwa Jamal
Bayser wamsajili Mtibwa Sugar- lakini kumbe wakati huo huo alikuwa ana
makubaliano na wakala mmoja ampeleleke India.
![]() |
| Mwenyekiti wa Simba SC, Alhaj Ismail Aden Rage akionyesha mikataba yaoa na Yondan |
Alisaini Mtibwa, akachukua fedha na akatimkia India- hadi
leo mimi naogopa kuwaambia Mtibwa kuna mchezaji nataka niwaletee, kwa kitendo
alichofanya Pius. Nashukuru tu baadaye mchezaji huyo alirejea na kujiunga na
timu hiyo.
Victor Costa alisaini Yanga akitokea Simba, akavaa jezi
kwenye Kombe lsa Mapinduzi Zanzibar, aliporejea Dar es Salaam akaenda kwenye
mazoezi ya Simba Kurasini, mwaka 2005. Amri Said alisaini Yanga mwaka 2001,
lakini pamoja na kupewa fedha, akabaki Simba.
Ephraim Makoye Mahala alisaini Simba mwaka 2000, kwenye
ofisi za New Habari Media Group, wakati huo zikiitwa Habari Corporations
Limited kwa dili lililosukwa na mwandishi mmoja wa kike shabiki wa kufa wa
Simba, lakini akabaki Yanga- ingawa baadaye alicheza Simba.
Sioni sababu ya kuhamaki katika suala hili- haswa kwa
Waandishi wa Habari, bali wanatakiwa kwanza kujiridhisha na ukweli ndipo watoe
hukumu.
Yondan huyu mmoja alisema hajasaini Yanga amesaini Simba,
akasema tena hajasaini Simba amesaini Yanga. Kwa nini sasa tuhamaki na
kuendesha magari kwa visirani na hasira mwishoni tufanye ajali barabarani bure?
Ipo Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF, ipo
Kamati ya Nidhamu ya TFF, kutoka kwao tunatarajia watalipatia ufumbuzi suala la
Yondan. Baada ya hapo, tutakuwa na fursa nzuri ya kufungua mijadala mipya.
Nawasilisha.






.png)
0 comments:
Post a Comment