• HABARI MPYA

    Wednesday, June 27, 2012

    YANGA WABADILISHA PROGRAMU, UWANJA WA MAZOEZI


    Yanga wakijifua ufukweni 

    Na Prince Akbar
    KLABU ya Yanga imebadilisha programu ya mazoezi kutoka asubuhi hadi mchana na pia imehama Uwanja wa Kaunda hadi, Kijitonyoma huku ikiwa katika mpango wa kuhamia shule ya sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam.
    Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, Yanga imefanya mazoezi Uwanja wa Kijitonyama mchana na mpango wa kuhamia Loyola unaendelea.
    Awali, Yanga ilikuwa inafanya mazoezi asubuhi, lakini sasa makocha wa klabu hiyo, Freddy Felix Minziro na Msaidizi wake, Mfaume Athumani Samatta wamehamishia zoezi hilo mchana, ingawa haijajulikana kama programu hiyo itaendelea au la.
    Mabingwa hao watetezi wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame wapo kwenye maandalizi ya kutetea taji lao la michuano hiyo, ambayo inatarajiwa kuanza Julai 14 hadi 29, mwaka huu Dar es Salaam.
    Timu nyingine mbili za Tanzania zitashiriki michuano hiyo, ambazo ni mabingwa wa nchi, Simba SC na washindi wa pili wa Ligi Kuu, Azam FC.
    Yanga bado ipo kwenye mchakato wa kusaka Kocha Mkuu, baada ya mwishoni mwa msimu kumtupia virago Mserbia, Kostadin Bozidar Papic.
    Inaelezwa klabu hiyo ipo kwenye mazungumzo na kocha wa zamani wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mbrazil Marcio Maximo na wakati huo huo inazungumza na chaguo mbadala, kutoka Ulaya iwapo itamkosa mwalimu huyo aliyeiwezesha Taifa Strars kucheza fainali za CHAN mwaka 2009 nchini Ivory Coast.
    Yanga imefanya usajili wa kusisimua, ikiwanasa wachezaji nyota kama kipa Ally Mustafa ‘Barthez’, beki Kelvin Yondan, wote kutoka kwa mahasimu Simba SC, beki Ladislaus Mbogo kutoka Toto African, viungo Frank Damayo kutoka JKT Ruvu, Nizar Khalfan aliyekuwa anakipiga Marekani na mshambuliaji Simon Msuva kutoka Moro United.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WABADILISHA PROGRAMU, UWANJA WA MAZOEZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top