• HABARI MPYA

    Thursday, June 28, 2012

    AZAM WAHAMISHIA KAMBI ZANZIBAR


    Katibu wa Azam, Nassor Idrisa

    Na Prince Akbar
    AZAM FC, Washindi wa Medali ya Fedha ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, wanatarajiwa kuondoka nchini Jumapili kwenda visiwani Zanzibar kushiriki michuano ya Kombe la Ujirani Mwema, inayoandaliwa na Chama cha Soka Zanzabr (ZFA).
    Katibu wa Azam FC, Nassor Idrisa ameiambia BIN ZUBEIRY kwamba, wataondoka mapema asubuhi, tayari kucheza mechi ya ufunguzi dhidi ya U23 ya Zanzibar usiku wa siku hiyo, Uwanja wa Amaan, mechi ambayo itatanguliwa na mchezo wa ufunguzi kati ya Yanga na Jamhuri ya Pemba.
    Tayari wachezaji wote waliosajiliwa na Azam FC kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na michuano ya Afrika, wapo mazoezini, kasoro tu Salum Abubakar ‘Sure Boy Jr.’ pekee, ambaye ni majeruhi.
    Wachezaji waliokamilisha idadi ya kikosi kizima cha Wana Lamba Lamba ni kipa Deo Munishi ‘Dida’ na mshambuliaji John Bocco ‘Adebayor’, walioripoti jana, ambao walikuwa wana udhuru.
    Dhahiri sasa, maandalizi ya Azam FC kwa ajili klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame ni kama yameanza rasmi, huku Makocha Waingereza, Stewart Hall na Msaidizi wake, Kalimangonga Sam Daniel Ongala wakiwa wenye matumaini makubwa na kikosi chao.
    Sure Boy Jr. aliyeumia mazoezi timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars ikiwa inajiandaa na mechi dhidi ya Msumbiji wiki mbili zilizopita, anaendelea na programu maalum ya daktari wa timu hiyo na tayari ameripoti. 
    Azam, washindi wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara walikwishamalisha usajili wa wachezaji wao hata kabla ya kwenda likizo.
    Programu ya maandalizi ya Kombe la Kagame, inayoendelea hivi sasa itamalizika siku moja kabla ya kuanza mashindano hayo, Juni 28 na yatakapomalizika, wachezaji watapewa mapumziko ya siku chache kabla ya kuanza maandalizi kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu.
    Maandalizi kwa ajili ya VPL yatahusisha pia ziara ya nje ya nchi ya kujiandaa na msimu mpya, ingawa amesema nchi hiyo itatajwa baadaye.
    Wachezaji wapya kikosini Azam msimu huu ni kiungo Mkenya George ‘Blackberry’ Odhiambo na kipa Deogratius Munishi kutoka Mtibwa Sugar, wakati Aishi Salum, Jackson Wandwi, Dizana, Ibrahim Rajab Jeba na Joseph Kimwaga, wamepandishwa kutoka akademi ya Azam.
    Kikosi kamili cha Azam FC kinaundwa; na makipa, Mwadini Ally, Deo Munishi ‘Dida’ Aishi Salum na Jackson Wandwi, mabeki wa Ibrahim Shikanda, Erasto Nyoni, Waziri Salum, Samir Haji Nuhu, Luckson Kakolaki, Said Mourad, Joseph Owino na Aggrey Morris.
    Viongo ni Kipre Bolou, Abdulhalim Humud, Himid Mao, Salum Abubakar, Abdi Kassim Sadalla, Ramadhani Suleiman Chombo, Abdulghani Ghullam, Ibrahim Rajab Jeba, Jabir Aziz Stima, Ibrahim Joel Mwaipopo, Kipre Tchetche, Mrisho Ngassa, Zahoro Pazi, Khamis Mcha na George Odhiambo ‘Blackberry’ wakati washambuliaji ni Gaudence Mwaikimba, John Bocco ‘Adebayor’.
    Hii ni mara ya kwanza kwa Azam FC kucheza Kombe la Kagame, baada ya kushika nafasi ya pili katika msimu uliopita wa Ligi Kuu. Katika Kombe la Kagame mwaka huu, wenyeji Bara wataingiza timu tatu, Yanga ambao ni mabingwa watetezi, wakati Simba na Azam wanaingia kwa nafasi za uwakilishi.
    Michuano ya Kagame inatarajiwa kuanza Julai 14 hadi 29, mwaka huu na kuna uwezekano Azam FC wakachezea mechi zao kwenye Uwanja wao wa Chamazi, kuwa michuano hiyo itafanyika katika kituo kimoja tu, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM WAHAMISHIA KAMBI ZANZIBAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top