• HABARI MPYA

    Friday, May 29, 2020

    MAMBO YA KUZINGATIA MICHEZONI WAKATI WA MAAMBUKIZI YA CORONA

    Na Mwandishi Wetu, DODOMA
    UTANGULIZI; Kufuatia kuwepo kwa ugonjwa wa CoVID-19 unaotokana na Virusi vya Corona nchini ambao uliripotiwa kwa mara ya kwanza mwezi Machi, 2020, Serikali iliamua kusimamisha shughuli zote za michezo ikiwemo mashindano ya Ligi za Soka kwa lengo la kupunguza kuenea kwa ugonjwa huo. Takwimu za mwenendo wa ugonjwa wa CoVID-19 nchini kwa sasa zinaonesha kupungua kwa wagonjwa jambo ambalo linaleta matumaini ya kuendelea na shughuli za kijamii ikiwemo Serikali kupitia kwa Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kuruhusu shughuli za michezo kuendelea kuanzia Juni Mosi, 2020. Aidha, Mhe. Rais aliziagiza Wizara zenye dhamana ya Afya na ile ya Michezo kuandaa Mwongozo wa pamoja wa namna michezo itakavyorejea nchini hususani ligi za soka.
    Kwa maelekezo hayo, wataalamu na baadaye viongozi wa sekta hizi mbili, kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa michezo yakiwemo mabaraza, shirikisho, vyama na vilabu vyenyewe, wamekubaliana kuzingatiwa.

    Mambo ya Kuzingatia; Utaratibu huu unalenga kusaidia kuwepo kwa mazingira wezeshi na salama ili
    kuendelea na michezo na kuepusha kuenea kwa maambukizi ya Virusi vya Corona.
    Aidha utaratibu huu utatumika ndani ya Tanzania Bara kwa michezo ya aina zote na katika ngazi zote hususani Ligi Kuu ya Soka na michezo mingine mbalimbali. Katika kufanikisha uwepo wa mazingira hayo yafuatayo ni muhimu kuzingatiwa;-
    1
    2.0.1 Elimu kwa wadau wa michezo kuhusu kujikinga na maambukizi:
    a) Wataalam wa afya kwa kushirikiana na wasimamizi wa michezo husika watoe elimu kwa wadau wa michezo kuhusu kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona kabla michezo yote haijaanza rasmi ikiwemo kuhusu Mwongozo huu na maelekezo mengine ya wataalamu wa afya;
    b) Wataalamu wa afya waendelee kusambaza mabango kwenye viwanja, vyumba vya kubadilishia nguo, kambi za michezo kwa ajili ya wachezaji na mashabiki kusoma taratibu na kanuni za kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya Corona. Aidha mabango yawekwe pia katika maeneo yote yatakayohusisha wananchi kuangalia mashindano ya michezo;
    c) Kuweponamatangazoyamarakwamarandaninanjeyaviwanjavya michezo kabla, wakati na baada ya matukio ya michezo;
    d) Madaktari wa timu au washauri wa afya wa vyama na mashirikisho ya michezo washiriki katika hatua hizi kikamilifu kwa kutoa semina kwa wachezaji na viongozi kuhusu mambo ya kuzingatiwa kiafya katika kila hatua za maandalizi, kambi, mechi na baada ya mechi;
    e) Viongozi wengine wa vilabu, vyama, mashirikisho, timu kama vile Wenyeviti, wadhamini, wasemaji, Makatibu Wakuu, makocha na manahodha nao washiriki kikamilifu kutoa elimu na kusisitizia tatahdhari za kiafya kila wanapopata nafasi; na
    f) Matangazo na machapisho yote yazingatie pia kuwezesha makundi yenye mahitaji maalum kupata elimu husika.
    2.0.2 Kambi, Viwanja vya Mazoezi na Mechi
    i. Uongozi wa viwanja na vyama/shirikisho husika waweke miundimbinu ya kuwezesha upatikanaji wa maji tiririka na sabuni kwa ajili ya kunawia mikono au vipukusi (sanitizers) katika maeneo yote muhimu kwa ajili ya kujikinga na maambukizi;
    2
    ii. Milango yote ya kuingiza watu viwanjani ifunguliwe mapema na itumike kwa kuzingatia umbali wa mita moja wakati wa kuingia na kutoka ili kuepusha misongamano;
    iii. Katika mazingira ambapo watazamaji wataruhusiwa kuingia viwanjani ukaaji uzingatie umbali wa mita moja baina ya mtu na mtu. Uongozi wa viwanja, vyombo vya dola na wasiwamizi wengine wa ligi waruhusu tu watazamaji watakaokuwa tayari kuzingatia na kutii Kanuni za afya na kuchukua hatua kali dhidi ya wale watakaokaidi ikiwemo kuwatoa uwanjani au kuzuia wasihudhurie tena mechi;
    iv. Mashabiki, viongozi na wadau wote wanaohusika na mechi wakiwemo wanahabari watalazimika kuvaa barakoa kwa muda wote wawapo uwanjani;
    v. Viongozi wa vilabu uhakikishe wachezaji wanajisafisha kwa vipukusi au maji tiririka kwa ajili ya kujikinga na maambukizi kabla na baada ya mechi/mazoezi;
    vi.Uongozi wa viwanja kwa kushirikiana na mashirikisho/vyama/timu mwenyeji waweke vifaa vya kuhifadhi taka pamoja na maji safi na salama katika vyoo wakati wote hasa wakati wa mazoezi na mashindano;
    vii.Wasimamizi wa michezo husika wahakikishe kunakuwepo na gari la wagonjwa lenye vifaa muhimu ikiwemo vifaa vya kusaidia kupumua kwa ajili ya tahadharI hasa katika michezo inayohusiska wachezaji na mashabiki wengi kama soka n.k;
    viii. Kila uwanja utenge maeneo ya tahadhari kwa ajili ya washukiwa wa CoVID-19 iwapo watabainika watu wenye dalili za ugonjwa huo na kuhitaji kutengwa kabla ya vipimo;
    3
    ix. Kabla ya kuingia uwanjani kwa ajili ya mazoezi na/au mechi wachezaji na viongozi wa kwenye benchi la ufundi na viongozi wengine wapimwe joto au kuona kama wanadalili nyingine zozote za CoVID -19;
    x. Mchezaji au kiongozi atakayeonesha dalili za kutia shaka atazuiwa kuungana na wenzake, kutengwa na kuelekezwa namna ya kwenda kupata vipimo kamili na ataruhusiwa kujiunga baada ya kuthibitika kuwa hana CoVID-19;
    xi. Utakuwa ni wajibu wa madaktari wa kila timu na wataalamu wengine wanaokuwepo katika michezo mbalimbali kusimamia Kanuni hizi wakati wote wachezaji wanapokuwa kambini, safarini, mazoezini au viwanjani na hatua kali zitachukuliwa kwa wataalamu hao iwapo kutabainika kuzembea katika usimamizi;
    xii. Wenye viti na watendaji wa mitaa/vijiji waendelee kusimamia maeneo ya mashabiki kutazama michezo na kutoruhusu maeneo hatarishi kama vile “vibanda umiza” au baa mbalimbali kuonyesha michezo bila kuzingatia kanuni za afya kama vile watu kutakiwa kunawa kwa maji tiririka au vipukusi kabla ya kuingia maeneo hayo na kuzingatia ukaaji wa mita moja kutoka mtu mmoja hadi mwingine.
    2.0.3 UsalamawaWachezajinaViongozi;
    i. Kabla ya Ligi hasa za Soka, Mpira wa Pete, Mpira wa Kikapu, Masumbwi na michezo mingine yenye mashabiki au wachezaji wengi; wachezaji na viongozi wote wa mabenchi ya ufundi wapimwe afya zao isipokuwa tu iwapo wahusika hawana dalili zozote za CoVID-19 au hawajatoka kwenye nchi nyingine za nje zenye maambukizi ya ugonjwa huo ili kujiridhisha na afya zao kabla ya kuingia kambini. Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Waganga Wakuu wa Mikoa/ Wilaya husika watasimamia zoezi hili;
    ii. Aidha utaratibu wa kuwapima joto wachezaji na viongozi wengine wanaosimamia timu kila siku za mazoezi na mechi uzingatiwe kwa kusimamiwa na madaktari wa timu husika na wataalamu wengine wa Afya;
    4
    iii. Wachezaji na viongozi watakaohisiwa/watakaojihisi kuwa na dalili za kuumwa ugonjwa wa Corona watoe taarifa ili waunganishwe na vituo vya matibabu na washiriki tu katika michezo pale hali zao zitakapoimarika.
    2.0.4 Mazingira Mengine Wakati wa Mazoezi na Mashindano
    i. Iwapo kutakuwa na ruhusa ya kuingia viwanjani, mashabiki hawataruhusiwa kusababisha misongamano wakati wa kuingia viwanjani au ushangiliaji kabla, wakati na baada ya mechi. Wasimamizi wa ligi watachukua hatua kali iwapo kuna mashabiki au wachezaji wa timu itakayokiuka maagizo haya. Aidha, vilabu ambavyo mashabiki wao watakiuka hatua hizi vichukuliwe hatua kwa mujibu wa Kanuni za Ligi;
    ii. Inasisitizwa wachezaji kutopeana mikono, kupongezana kwa kukumbatiana na kubadilishana jezi kabla, wakati na hata baada ya mazoezi na mechi;
    iii. Inaelekezwa kuwa wachezaji na viongozi wanaokaa kwenye benchi la akiba wazingatie kanuni ya mita moja kuliko kubanana kama ilivyo katika mfumo wa kawaida;
    iv. Mahojiano kati ya viongozi, wachezaji na wadau wengine wa michezo mazoezini au viwanjani kabla na baada ya mechi yazingatie Mwongozo wa Kuripoti Habari wakati wa CoVID-19 unaoelekeza kujiepusha na mambo mbalimbali ikiwemo kuzingatia umbali wa mita moja kati ya wahusika na kuangaliwa njia zaidi za kidijiti kuliko mahoniano ya ana kwa ana na wanahabari kuhakikisha wametakasa vifaa vyao na kutowashikisha kifaa chochote wahojiwa ili kuzilinda pande zote;
    v. Wakati wa kusafiri viongozi na wachezaji wazingatie taratibu zote za kujikinga ikiwemo kuhakikisha abiria wote wamekaa kwenye viti na kunawa kwa maji tiririka au vipukusi kabla ya kuingia kwenye vyombo vya usafiri;
    vi. Watu walio katika hatari zaidi ya maambukizi kama vile wazee, watu wenye magonjwa sugu na magonjwa ya muda mrefu wanashauriwa kutohudhuria
    5
    viwanjani na badala yake waelekezwe kutazama michezo kupitia televisheni wakiwa nyumbani au kusikiliza kwenye redio au kwenye maeneo yasiyo na mikusanyiko.
    2.0.5 Vifaa vya michezo:
    i. Vifaa na nyenzo zote zinazotumika wakati wote wa michezo vitatakiwa kusafishwa vyema kwa vipukusi au maji tiririka na sabuni kabla na baada ya mazoezi au mechi. Aidha kwa vifaa ambavyo vitaingizwa kutoka nje ya nchi kwa shughuli za michezo vinalazimika kuthibitishwa usalama wake na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) na Bohari ya Dawa (MSD) kabla ya kusambazwa na kuanza kutumika nchini;
    ii. Vyama mbalimbali vya michezo vinavyoendelea kurejesha michezo mbalimbali vitalazimika kuwasilisha mipango yao kwa BMT na Baraza litashirikisha Waganga Wakuu wa Mikoa/ Wilaya ili kujiridhsiha na namna michezo husika itakavyozingatia Kanuni za Afya na Miongozo mbalimbali ya Afya wakati huu wa CoVID-19 kabla ya kutoa idhini ya kuendelea kwa michezo hiyo;
    iii. Serikali kupitia BMT, baada ya kushauriana na wataalamu wa afya, inaweza kutoa maelekezo mengine mahsusi zaidi ya haya kulingana na hali halisi itakavyokuwa ikijitokeza viwanjani au sehemu nyingine za michezo na maelekezo hayo yatapaswa kutekelezwa ipasavyo;
    iv. Hatua kali zichukuliwe kwa mujibu wa Sheria za nchi, Sheria inayounda BMT, Kanuni za Ligi mbalimbali zinazosimamia michezo mbalimbali kwa mashirikisho, vyama, viongozi, wachezaji, vilabu au mashabiki na wadau wengine wa michezo watakaokiuka mwongozo huu.
    3.0 Mawanda na Kuanza Kutumika Mwongozo:
    Mwongozo huu unaohusu Kanuni Muhimu za Kiafya za kuzingatiwa wakati huu wa uwepo wa maambukizi, japo machache, ya ugonjwa wa CoVID-19 hapa nchini, utahusu michezo yote inayoendelea kurejea Tanzania Bara inayoendeshwa na vyama, mabaraza, Kamati, Vilabu au Mashirikisho na asasi nyingine zozote zilizosajiliwa na BMT.
    Halikadhalika, Mwongozo huu utakoma kutumika mara tu Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakapotangaza kuwa hakuna ugonjwa CoVID-19 nchini, pia utaanza kutumika rasmi kuanzia tarehe ya kusainiwa iliyoainishwa hapa chini.
    (Waraka huu umesainiwa Waziri Wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee Na Watoto, Ummy Ally Mwalimu Waziri Wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison George Mwakyembe)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAMBO YA KUZINGATIA MICHEZONI WAKATI WA MAAMBUKIZI YA CORONA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top