• HABARI MPYA

    Saturday, February 20, 2016

    MRISHO MPOTO, KAYUMBA KUPAMBA UZINDUZI WA BENDI MPYA DAR

    Na Somoe Ng'itu, DAR ES SALAAM
    BENDI mpya ya muziki wa dansi ya BMM inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Ijumaa katika onyesho lililopangwa kufanyika kwenye ukumbi wa Millenium Tower, Makumbusho jijini Dar es Salaam.
    Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, kiongozi wa bendi hiyo, Mule Mule, alisema kuwa maandalizi ya utambulisho wa BMM yamekamilika na watatumia siku hiyo kukitambulisha kibao chao kipya kiitwacho 'Watabiri'.
    Mule Mule ambaye amejiunga na bendi hiyo akitokea FM Academia 'Wazee wa Ngwasuma' alisema kuwa wasanii mbalimbali watasindikiza uzinduzi wa bendi hiyo na kuwataja baadhi yao kuwa ni Mrisho Mpoto, Barnaba na mshindi wa BSS mwaka jana, Kayumba.
    Toto Ze Bingwa (kushoto) akizungumza leo. Katikati ni Mule Mule na kulia ni Mkurugenzi wa BMM, Deus Macha

    Alisema kwamba bendi hiyo imejipanga kuleta mapinduzi ya muziki wa dansi Tanzania na kurudisha heshima ya muziki huo kama zilivyokuwa zikitamba Msondo Ngoma na Sikinde.
    "Inasikitisha sana kuona Diamond ndiyo anampa zawadi ya gari (Muhidin) Gurumo (marehemu), badala ya Gurumo kumpatia Diamond, tumejipanga, ujio wetu mpya tunaamini Watanzania watatupokea tukiwa na sura mpya, tunataka kuona mapinduzi ya muziki yanaoneka kwa wasanii wakongwe tunasaidia chipukizi," alisema Toto ze Bingwa ambaye pia ni mwanamuziki wa bendi hiyo.
    Mmiliki wa bendi hiyo, Deus Macha alisema kwamba amejiandaa kuwekeza kuinua wasanii chipukizi na kwa muda huu hatajali kiasi cha fedha atakachotumia.
    (Somoe Ng'itu ni mwandishi wa gazeti la Nipashe)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MRISHO MPOTO, KAYUMBA KUPAMBA UZINDUZI WA BENDI MPYA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top