• HABARI MPYA

    Tuesday, July 29, 2014

    TP MAZEMBE NA AS VITA ZAKABANA KOO KILELENI KUNDI A LIGI YA MABINGWA, WAARABU WAJIKOKOTA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    KLABU za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), TP Mazembe ya Lubumbashi na AS Vita ya Kinshasa zinakabana koo kileleni mwa Kundi A katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Baada ya mechi za kwanza za mzunguko wa pili wa kundi hilo, kila timu imefikisha pointi saba na zote zina wastani wa bao moja baada ya kutoa mabao ya kufunga na kufungwa.
    Mazembe yenye washambuliaji wawili Watanzania, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu ilianza mzunguko wa pili kwa sare ya bila kufungana ugenini mjini Cairo dhidi ya wenyeji, Zamalek jana, wakati AS Vita ilianza na ushindi wa mabao 2-1 nyumbani jana dhidi ya Al Hilal ya Sudan.
    Baada ya mechi nne, kila timu sasa kati ya Mazembe na Vita imeshinda mechi mbili na kutoa sare moja pamoja na kufungwa mechi moja moja. Vita imefunga mabao matano na kufungwa manne, wakati nyavu za timu ya akina Samatta zimetikiswa mara moja wakati yenyewe imefunga mabao mawili. 
    Hilal na Zamalek zote zina pointi nne kila moja baada ya mechi nne, zimefungwa zaidi bao moja kuliko zilivyofunga kila moja.
    Kwa upande wa Kundi B, juzi CS Sfaxien iliibwaga bao 1-0 Esperance, zote za Tunisia, wakati Al Ahly Benghazi ya Libya ilifungwa nyumbanai mabao 2-0 ES Setif ya Algeria.
    Setif yenye pointi nane za mechi nne ipo kileleni mwa Kundi B, ikifuatiwa na Sfaxien yenye pointi saba, Benghazi pointi nne na Esperance pointi tatu.
    Jumamosi hii michuano hiyo itaendelea, TP Mazembe ikiikaribisha Al Hilal Lubumbashi, Zamalek ikiwa mwenyeji wa AS Vita Cairo, Al Ahly Benghazi ikiikaribisha CS Sfaxien na ES Setif ikiwa mwenyeji wa Esperance.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TP MAZEMBE NA AS VITA ZAKABANA KOO KILELENI KUNDI A LIGI YA MABINGWA, WAARABU WAJIKOKOTA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top