• HABARI MPYA

    Sunday, November 29, 2015

    ETOILE DU SAHEL NDIYO MABINGWA WA KOMBE LA SHIRIKISHO 2015

    ETOILE du Sahel ya Tunisia imetwaa ubingwa wa Kombe la Shirikisho Afrika (CAF) baada ya leo kuifunga bao 1-0 Orlando Pirates ya Afrika Kusini Uwanja wa Olimpiki mjini Sousse.
    Shukrani kwake, mfungaji wa bao hilo pekee, Ammar Jemal amablo linaifanya Etoile itwae taji hilo kwa ushindi wa jumla wa 2-1 baada ya sare ya 1-1 katika mchezo wa kwanza Jumamosi iliyopita mjini Soweto.
    Jemal, mwenye umri wa miaka 28, beki wa kati ambaye amecheza Uswisi, Ujerumani, Ufaransa na Saudi Arabia, pia alifunga katika mchezo wa kwanza Afrika Kusini na kuwa na mchango mkubwa kwa klabu hiyo kutwaa taji la tisa la CAF.

    Kona fupi ilifuatiwa na krosi ambayo ilimshinda Nahodha wa Pirates, Happy Jele na kipa wake, Felipe Ovono akashindwa kuokoa na kumuacha Jemal afunge kiulaini.
    Jemal amefikisha mabao matano katika mechi 16 za Kombe la Shirikisho alizocheza na kuwa mfungaji bora wa pili wa Mashetani hao Wekundu, nyuma ya Baghdad Bounedjah mwenye mabao sita.
    Ikumbukwe Etoile iliitoa Yanga SC ya Tanzania kwa mbinde katika hatua ya 16 Bora ya michuano hiyo kwa ushindi wa jumla wa 2-1 baada ya sare ya 1-1 ya Dar es Salaam na ushindi wa 1-0 mjini Sousse.
    Sasa Etoile itamenyana na TP Mazembe ya DRC, mabingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika kuwania taji la Super Cup la CAF.    
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ETOILE DU SAHEL NDIYO MABINGWA WA KOMBE LA SHIRIKISHO 2015 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top