• HABARI MPYA

    Tuesday, January 24, 2017

    SENEGAL WAITUPA NJE ALGERIA AFCON 2017

    ALGERIA imetolewa mapema katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya sare ya 2-2 jana na Senegal mjini Franceville katika mchezo wa mwisho wa Kundi B.
    Pamoja na mshambuliaji wa mabingwa wa England, Leicester City, Islam Slimani kufunga mabao mawili dakika za 10 na 52, haikuisaidia Algeria kusalia kwenye michuano baada ya Senegal kusawazisha kupitia kwa Papa Diop dakika ya 43 na Moussa Sow dakika ya 53, Simba wa Teranga wakimaliza kileleni mwa Kundi B.
    Tunisia imeungana na Senegal kwenda Robo Fainali kutoka Kundi hilo baada ya ushindi wa 4-2 dhidi ya Zimbabwe mjini Libreville jana wakiweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kufunga mabao manne katika mechi moja kwenye AFCON ya mwaka huu.
    Kipa wa Senegal, Khadim N'Diaye (katikati) akiruka kudaka dhidi ya wachezaji wa Algeria huku akilindwa na mabeki wake jana

    Mabao ya Tunisia yalifungwa na Naim Sliti dakika ya tisa, Youssef Msakni dakika ya 22, Taha Yassine Khenissi dakika ya 36 na Wahbi Khazri dakika ya 45 kwa penalti wakati ya Zimbabwe yalifungwa na Knowledge Musona dakika ya 42 na Tendai Ndoro aliyetokea benchi dakika ya 58.
    Senegal wanamaliza kileleni mwa Kundi B kwa pointi zao saba, wakifuatiwa na Tunisia iliyomaliza na pointi sita, Algeria pointi mbili na na Zimbabwe moja.
    Michuano hiyo inaendelea leo kwenye mechi za Kundi C, mabingwa watetezi, Ivory Coast wakimenyana na Morocco Uwanja wa d'Oyem na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wakimenyana na Togo Uwanja wa Port Gentil, mechi zote zikianza Saa 4:00 usiku.
    Hadi sasa DRC inaongoza Kundi C kwa pointi zake nne, ikifuatiwa na Morocco pointi tatu, Ivory Coast pointi mbili na Togo pointi moja. 
    Maana yake nafasi zote mbili za kufuzu Robo Fainali kutoka kundi hilo bado zipo wazi kwa timu zote, kwani hata Togo ikishinda kwa wastani mzuri wa mabao inaweza kufuzu pia matokeo ya mechi nyingine yakiruhusu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SENEGAL WAITUPA NJE ALGERIA AFCON 2017 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top