• HABARI MPYA

    Sunday, September 22, 2013

    YANGA WACHARAZWA NA AZAM...KINDA LA B CHAMAZI LAWAFUNGA MIDOMO TAIFA

    Na Mahmoud Zubeiry, IMEWEKWA SEPTEMBA 22, 2013 SAA 12:18 JIONI
    AZAM FC imefanikiwa kufuta uteja kwa Yanga SC leo baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-2 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Shujaa wa Azam leo, alikuwa ni kinda aiyepandishwa kutoka kikosi cha pili, Joseph KImwaga ambaye alifunga bao la tatu kwa umahiri mkubwa, baada ya kuuwahi mpira mrefu na kuwazidi mbio mabeki wa Yanga kabla ya kumchambua kipa Ally Mustafa ‘Barthez’ dakika ya 90.
    Lilikuwa bao la kumaliza mchezo na wachezaji wote wa Azam walikwenda kumpongeza Kimwaga nje ya Uwanja upande wa lango la Yanga na waliporejea uwanjani, baada ya dakika moja na ushei filimbi ya kuhitimisha mechi ilipulizwa. 
    Mshindi wa mechi; Wachezaji wa Azam FC wakiwa wamembeba Joseph Kimwaga baada ya kufunga bao la ushindi

    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Dominic Nyamisana, aliyesaidiwa na Charles Simon na Flora Zablon wote wa Dodoma, hadi mapumziko, Azam walikuwa mbele kwa bao 1-0.
    Bao hilo lilifungwa na John Bocco ‘Adebayor’ sekunde ya 34 tu, baada ya kuuwahi mpira uliorudishwa na beki Kevin Yondan kufuatia pigo la kichwa la Brian Umony na kuutumbukiza nyavuni. 
    Yanga SC inayofundishwa na Mholanzi, Ernie Brandts, ilikuja juu baada ya bao hilo na kufanya mashambulizi mengi langoni mwa Azam, lakini hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika hawakufanikiwa kupata bao.
    Lakini kipindi cha pili, Yanga walirudi na moto mkali na kufanikiwa kusawazisha bao dakika ya 48 kupitia kwa Mrundi, Didier Kavumbangu aliyeutokea mpira mrefu na kwenda kumchambua kipa wa Azam, Aishi Manula.  
    Yanga iliongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa Azam na kufanikiwa kupata bao la pili, dakika ya 65 mfungaji Hamisi Kiiza aliyemalizia pasi ya Simon Msuva.
    Huzuuni; Mshambuliaji wa Yanga Jerry Tegete akiwa mwenye huzuni baada ya Azam kupata bao la tatu, huku dakika zikiyoyoma

    Yanga walijiona kama wamemaliza kazi baada ya bao hilo na haikushungaza kibao kilipowageukia na kulala katika mchezo huo.
    Beki Kevin Yondan aliunawa mpira kwenye eneo la hatari dakika ya 68 na Kipre Herman Tchetche akaenda kufunga kwa penalti dakika ya 69 na kufanya 2-2.
    Yanga wakazinduka na kuongeza mashambulizi langoni mwa Azam kusaka bao la ushindi, lakini shambulizi la kushitukiza la Wana Lamba Lamba liliwamaliza Wana Jangwani dakika ya 90.
    Azam waliokoa shambulizi la hatari langoni mwao na kuanzisha shambulizi la haraka- na mchezaji bora wa michuano ya Kombe la Uhai msimu uliopita, Kimwaga hakufanya makosa- hadi mwisho Azam 3-2 Yanga.
    Kwa ujumla mchezo ulikuwa mkali na mashambulizi yalikuwa ya pande zote mbili. Huu unakuwa ushindi wa pili kwa Azam msimu huu ndani ya mechi tano na sasa inafikisha pointi tisa, wakati kwa Yanga SC hiki ni kipigo cha kwanza ndani ya mechi tano, wakiwa pia wametoa sare tatu na kushinda mechi moja, hivyo wanabaki na pointi zao sita.
    Katika mchezo huo, kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Simon Msuva, Frank Domayo, Didier Kavumbangu, Jerry Tegete/Hamisi Kiiza dk58 na Haruna Niyonzima.
    Azam FC; Aishi Manula, Erasto Nyoni, Waziri Salum, David Mwantika, Joackins Atudo/Said Mourad dk56, Himid Mao, Farid Mussa/Joseph Kimwaga dk72, Kipre Balou, John Bocco, Humphrey Mieno na Brian Umony/Kipre Tchetche dk52.  
    Katika mechi nyingine za ligi hiyo, JKT Ruvu ilifungwa 1-0 na JKT Oljoro Uwanja wa Azam Complex, bao pekee la Paul Malipesa dakika ya 79, Ruvu Shooting ililala 1-0 mbele ya Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, bao pekee la Haruna Moshi ‘Boban’ dakika ya 82.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: YANGA WACHARAZWA NA AZAM...KINDA LA B CHAMAZI LAWAFUNGA MIDOMO TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top