• HABARI MPYA

    Wednesday, September 18, 2013

    KASEJA ATUA ASHANTI UNITED KUGOMBEA NAMBA NA AMANI SIMBA

    Na Prince Akbar, IMEWEKWA SEPTEMBA 18, 2013 SAA 5:08 ASUBUHI 
    NAHODHA wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars Juma Kaseja amejiunga na timu ya Ashanti United ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na anatarajiwa kuanza kuichezea rasmi Januari mwakani, baada ya kuchelewa dirisha la usajili. 
    Kocha wa makipa wa timu hiyo ya Ilala, Dar es Salaam, Iddi Pazi ‘Father’ ameiambia BIN ZUBEIRY jana kwamba Kaseja amejiunga na Ashanti United na amekwishaanza kazi.
    Father, alisema kwamba pamoja na Kaseja, pia Ashanti imempata kipa mwingine mzoefu, Amani Simba SC ambaye naye amekwishaanza mazoezi.
    Ametua kwa wauza mitumba wa Ilala; Juma Kaseja amejiunga na Ashanti United

    “Nipo na Amani Simba na Juma Kaseja hapa Ashanti, naamini wote ni makipa wazuri na watachuana ili kurejea matawi ya juu. Nitawafanyia kazi na watakuwa makipa bora tena,”alisema Pazi, baba wa mshambuliaji wa Simba SC, Zahor Pazi.
    Kaseja aliachwa Simba SC mwishoni mwa msimu baada ya kuitumikia timu hiyo tangu mwaka 2003 alipojiunga nayo akitokea Moro United.
    Baada ya hapo, alipata ofa ya kwenda St. Eloi Lupopo ya DRC, lakini wakashindwa kuafikiana na kuamua kuangalia ustaarabu mwingine. Wakati wa maandalizi ya msimu mpya, Kaseja alikuwa akifanya mazoezi na Mtibwa Sugar iliyokuwa imeweka kambi Dar es Salaam.
    Juhudi za kumpata Kaseja mwenyewe kuthibitisha kujiunga kwake na Ashanti hazikuweza kufanikiwa mapema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: KASEJA ATUA ASHANTI UNITED KUGOMBEA NAMBA NA AMANI SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top