• HABARI MPYA

    Tuesday, September 17, 2013

    KAKA MKUU CHUJI ADHIBITI KOROSHO TBL MBEYA, NGASSA NA TEGETE WAWA WAPOLE

    Na Mahmoud Zubeiry, Mbeya, IMEWEKWA SEPTEMBA 17, 2013 SAA 2:56 ASUBUHI 
    YANGA SC inaye Nahodha, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, lakini pia inaye ‘Kaka Mkuu’, Athumani Iddi ‘Chuji’-  ni hatari tupu.
    Kaka Mkuu wa Yanga SC, Chuji jana alilazimika kuzuia vibakuli sita vya korosho vikiwemo vitano vya wachezaji wenzake, ili wasile kwanza wasikilize hotuba wakati wa ziara ya timu hiyo kiwanda cha kampuni ya Bia Tanzania (TBL) mjini hapa.
    Wachezaji waliokumbwa na kasheshe hilo ni pamoja na Jerry Tegete na Mrisho Ngasasa waliokuwa wameketi jirani na Kaka Mkuu wao.
    Zimedhibitiwa na Kaka Mkuu; Vibakuli vya korosho havitoki hadi hotuba ziishe

    Baada ya vibakuli vya korosho kupelekwa, Chuji akavichukua; “Dada yangu hivi viweke kwanza hapa hawa vijana wasikilize hotuba, ikiisha watakula,”alisema.
    Wachezaji hao ilibidi wawe wapole mbele ya amri ya Kaka Mkuu, lakini hawakuonekana kufuatilia hotuba yoyote kati ya zilizokuwa zikitolewa zaidi ya kucheza na simu zao za ‘bei mbaya’.
    Chuji alikuwa akisikiliza kwa makini hotuba zote mwanzo hadi mwisho. Baada ya hotuba hizo, ndipo Chuji akamgawia kila mmoja bakuli lake la korosho na kwa kuwa muda wa kuanza kutembelea kiwanda ulikwishawadia ilibidi wale huku wanatalii TBL Mbeya.
    Kikosi cha Yanga jana mchana kilifanya ziara kiwanda cha TBL hapa Mbeya, kilichopo maeneo Iyunga. Katika ziara hiyo, wachezaji walipata fursa ya kujionea mambo mbalimbali, ikiwemo mfumo mzima wa utayarishwaji bia hadi kupakiwa tayari kuingia sokoni.
    Chuji akisikiliza hotuba kwa makini, Ngassa na Tegete wanacheza na simu zao

    Walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali wakati wanatembezwa kwenye kiwanda hicho na wafanyakazi wa TBL Mbeya na kwa ujumla ilikuwa ziara yenye maufaa kwao. 
    Wafanyakazi wa TBL Mbeya walifurahi kukutana na wachezaji wa Yanga na wengine walichukua fursa hiyo kupiga nao picha za ukumbusho.
    Kwa upande wake, Meneja Matukio wa Kampuni hiyo mjini hapa, Godfrey Mwangungula alisema kwamba kiwanda cha TBL Mbeya kinashikilia tuzo ya kiwanda bora Afrika kwa miaka mitatu mfululizo- hivyo ni faraja kwao kutembeleaa na mabingwa wa Tanzania.
    Yanga kwa pamoja na wapinzani wao wa jadi, Simba SC na timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars- wote wanadhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premiem Lager inayozalishwa na TBL.
    Yanga iko hapa Mbeya tangu Jumatano kwa ajili ya mechi zake mbili za Ligi Kuu dhidi ya timu za hapa. Mchezo wa kwanza ilicheza Jumamosi Uwanja wa Sokoine na kulazimishwa sare ya 1-1 na Mbeya City wakati kesho itahitimisha mechi zake za hapa kwa kumenyana na Prisons kwenye Uwanja huo huo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: KAKA MKUU CHUJI ADHIBITI KOROSHO TBL MBEYA, NGASSA NA TEGETE WAWA WAPOLE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top