• HABARI MPYA

    Friday, March 27, 2009

    SIMBA YAPUMULIA MASHINE, YANGA CHEREKO

    Mwenyekiti wa Simba, Hassan Dalali akiwa Mussa Mgosi


    WAKATI Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara ikikaribia ukingoni, matumaini ya timu ya Simba kuwakilisha nchi katika michuano ya kimataifa mwakani bado yapo shakani. Kulingana na msimamo ulivyo wa ligi hiyo, baada ya Yanga kufanikiwa kutetea ubingwa kwa kufikisha pointi 46, vita inaonekana ipo zaidi katika nafasi ya pili, ambayo timu itakayoishika itashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho mwakani. Simba hadi sasa ipo nafasi ya pili ikiwa na pointi 27, sawa na Kagera Sugar inayoshika nafasi ya tatu zote zikilingana pointi, lakini Simba ina uwiano mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa. Kihesabu Yanga na Azam ndiyo zinaweza angalau kuiweka Simba katika nafasi nzuri kulingana na michezo yao itakayofanyika mwishoni mwa wiki. Yanga kesho inacheza na Kagera Sugar Uwanja wa Uhuru, zamani Taifa mjini Dar es Salaam, mchezo ambao mashabiki wa Simba kama wanaitakia mema timu yao icheze michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika (CAF), itabidi waishangilie Yanga iifunge Kagera. Kama Kagera Sugar ikifungwa kesho, kisha Simba ikaifunga Azam FC Jumapili kwenye uwanja huo huo, angalau itakuwa imeweka hai zaidi matumaini yake ya kuikwaa nafasi hiyo. Simba ambayo msimu uliopita ilikosa kuiwakilisha nchi kwenye michuano miwili mikubwa ya Ligi ya Mbaingwa Afrika na Kombe la Shirikisho, itakuwa ikitumaini kubebwa na watani zao wa jadi, ambao juzi Katibu Mkuu wa Yanga, Lucas Kisasa alikaririwa na gazeti hili akisema licha ya kutwaa ubingwa hawatakubali kupoteza mchezo wowote. Kama kauli ya Kisasa itatimia ni wazi itakuwa raha ya Simba, maana mpinzani wake wa karibu atakuwa amepunguzwa nguvu, lakini kama Yanga itafungwa, hali haitakuwa nzuri zaidi kwa Simba inayonolewa na Mzambia Patrick Phiri. Simba ina mabao 22 ya kufunga wakati Kagera ina mabao 15, timu hizo mbili kila moja imetoka sare michezo mitatu na kushinda nane. Lakini matokeo ya mchezo wa kesho bado yatakuwa na maana zaidi kama Jumapili Simba itaifunga Azam ambayo nayo pia haipo salama kwani ipo chini katika balaa la kushuka daraja ikiwa na pointi 22. Mchezo wa Simba na Azam hautakuwa mwepesi, ukizingatia matokeo ya hivi karibuni ya Azam kuichapa mabao 6-2 Villa Squad, hivyo nayo ni wazi itakuwa inawania kujiweka kwenye nafasi nzuri na kujiepusha na hatari ya kuwemo kwenye orodha ya timu zitakazoshuka daraja. Simba baada ya mchezo na Azam itakuwa imesaliwa na michezo minne dhidi ya Kagera Sugar, utakaofanyika Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, kisha Toto African, Yanga na na Polisi Dodoma. Lakini nafasi ya pili si tu inawaniwa na Simba na Kagera, bali pia inafukuziwa na timu nyingine ambazo zinaweza kuikwaa kama Simba na Kagera zikiteleza. Timu ambazo zinafukuzia nafasi hiyo ya pili ni Mtibwa na Prisons zenye pointi 25 kila moja na JKT Ruvu na Toto Africans zenye pointi 24 kila moja. Kila timu ina michezo mitano mkononi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAPUMULIA MASHINE, YANGA CHEREKO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top