• HABARI MPYA

    Friday, March 20, 2009

    SERIKALI YAMUWEKEA MKWARA MAXIMO, YASEMA AKIBORONGA ATATUPIWA VIRAGO

    Kikosi cha Stars kilichoshiriki CHAN


    NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Joel Bendera amesema endapo kocha wa Taifa Stars, Marcio Maximo atashindwa kufanya kile Watanzania wanataka, atakatizwa mkataba na atatimuliwa.
    Bendera alikuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu sababu za Serikali kuongeza mkataba na kocha huyo ambaye akifanya vizuri ataongezewa mkataba.
    Maximo ameongezewa mkataba baada ya ule wa awali wa miaka miwili kumalizika. Mkataba wake unamalizika Julai mwaka huu. Kutokana na hali hiyo, mkataba wake sasa utamalizika 2010.
    Awali Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, George Mkuchika alisema serikali imeridhishwa na kazi ya kocha huyo hata kukubali kuongeza mwaka mmoja zaidi wa mkataba wake.
    Mkuchika alisema kuwa bado wana imani na kocha huyo kutokana na rekodi yake, ambapo Stars chini ya Maximo ilicheza mechi 44 za mashindano na kirafiki na kati ya hizo ilishinda 20, sare 13 na kufungwa 11.
    Mkuchika alisema pia kuwa katika kipindi cha miaka 29 Tanzania hatukushiriki katika mashindano makubwa lakini Maximo aliiwezesha Taifa Stars kushiriki Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani, CHAN ambapo nchi nane zilishiriki.
    Alisema Maximo ameibua vipaji vya wachezaji chipukizi, amejenga nidhamu kwa wachezaji, ameongeza ari ya Watanzania kuipenda timu yao, amekuwa mbunifu wa vazi la timu ya taifa, ameitoa Stars nafasi ya 165 mpaka 101 na amewezesha wananchi kuishabikia timu ya taifa tofauti na miaka ya nyuma.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERIKALI YAMUWEKEA MKWARA MAXIMO, YASEMA AKIBORONGA ATATUPIWA VIRAGO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top