• HABARI MPYA

    Saturday, March 14, 2009

    Maximo aringia yosso alioachiwa na Tinocco

    Maximo akiwa na Kaseja


    KOCHA wa TaifaStars, Marcio Maximo amemsifu aliyekuwa msaidizi wake Marcus Tinoco kwa madai kwamba amemwachia vijana wenye umri mdogo lakini wenye vipaji vya hali ya juu.
    Tinoco alikuwa kocha mkuu wa timu za vijana kabla ya hivi karibuni kutimkia visiwa vya Trinidad $Tobago kwa ajili ya kuinoa timu ya klabu ya daraja la kwanza ya kulipwa nchini humo.
    Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Marcimo ambaye leo kikosi chake kitakwaana na Vancouver White Caps, mabingwa wa Ligi Kuu ya Amerika Kaskazini alisema Tanzania inapaswa kujivunia hazina kubwa ya wachezaji wenye umri mdogo na wenye vipaji walioachwa na Tinoco.
    Maximo ambaye kikosi chake cha sasa kimejaa wachezaji kutoka timu za vijana za miaka 20 na 17, alisema uwepo wa wachezaji wengi wa aina hiyo kutaifanya soka ya Tanzania kufikia mafanikio kama ya nchi za Nigeria na Angola.
    Akizungumzia mpambano wa leo kati ya vijana wake na Vancouver White caps, Mbrazili huyo alisema anatarajia kuwachezesha zaidi wachezaji vijana ili wapate uzoefu kwa vile baadhi yao hawana klabu na hawajawahi kucheza mechi zozote kubwa za ushindani.
    "Ninao wachezaji 15 wa umri kati ya miaka 20 na 17 nataka wapate uzoefu zaidi hawa kwani kuna ambao hawana klabu na hawajawahi kucheza mechi yoyote ya ushindani, lakini ninaamini wanajua kwanini wapo timu ya taifa na nini wajibu wao.
    "Natoa mfano kwa Razak Khalfan, Zahoro Pazi, John Bocco na Mwinyi Kazimoto hawa watakuwepo kwenye kikosi cha kwanza kitakachocheza leo. Ni wachezaji wazuri wanaohitaji uzoefu tu ili waje kuwa na msaada mkubwa kwa nchi ,"alisema.
    Aidha, Maximo aliwaomba wapenzi wa soka nchini wajitokeze kwa wingi kuwaunga mkono vijana wake na kukiri kuwa mpambano huo utakuwa mgumu kutokana na wageni kubadilika kimchezo tofauti walivyocheza na Yanga na kufungwa mabao 3-0 na juzi kuilaza Simba mabao 2-1.
    Hata hivyo, kocha huyo alitahadharisha kuwa ni vizuri wakayapokea matokeo ya aina yoyote na kuacha kuwakatisha tamaa vijana wake kwa vile ndio kwanza anawatengeneza.
    Naye kocha wa Vancouver White caps, Teitur Thordarson alikiri kuwa mpambano huo utakuwa mgumu kwavile wanacheza na timu ya taifa lakini akajigamba kuibuka na ushindi kwavile mazoezi ya kutosha na angalau wameozea hali ya hewa.
    "Najua mpambano utakuwa mgumu kwakuwa tunachea na timu ya taifa, nimecheza mechi mbili nimegundua hapa kuna wachezaji wenye vipaji na wenye kasi.
    Awali, tuliathiriwa na hali ya hewa kwa vile kule kwetu ni baridi kali hata hivyo tumefanya mazoezi sana na angalau tumezoea hali ya hapa hivyo nina imani ya kushinda mchezo,"alisema Thordarson.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: Maximo aringia yosso alioachiwa na Tinocco Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top