• HABARI MPYA

    Sunday, July 28, 2019

    UWEKEZAJI KATIKA KLABU TANZANIA UMEGUBIKWA NA SINTOFAHAMU

    Na Dominick Salamba, DAR ES SALAAM
    WASWAHILI wanamisemo sana na nimepata bahati ya kusikia misemo mingi mno baada ya kuingia na kuishi ukanda huu wa Pwani kule kwetu shinyanga hakuna sana misemo hii zaidi ya kukigonga kisukuma kwenda mbele.
    Moja ya misemo ambayo nimekutana nayo hapa mjini ingawa sikuja na gari la mkaa ni ule msemo wa SHAMBA LA BIBI ni msemo ambao sikuelewa lakini nilipo wauliza waungwana walio kulia pwani waliniambia kuwa huu msemo una maana kuwa shamba la bibi linakuwa huru kwa maneno mengine ni ruksa kuvuna chochote kwa kadri uwezavyo na hakuna mwenye uchungu nalo na ukiwa mjanja kuliko wengine ndio mahali unapoweza kupigia na kutoka kimaisha kwa misemo ya kimjini.Duuuh kumbe ndio hivi!
    Tuachane na hilo la shamba la bibi turudi kwenye mada yetu kuhusu uwekezaji katika soka letu na bila ubishi huwezi zungumzia soka la Tanzania bila kuhusisha vilabu viwili vikongwe hapa nchini YANGA SC na SIMBA SC ni kongwe kwani ndiyo timu za mwanzo kabisa kuanzishwa moja ikianza mwaka 1935 na nyingine 1936 na  ndizo zenye wapenzi na mashabiki wengi  katika nchini yetu na hata nchi za jirani hivyo nitajikita kuelezea nikilinganisha na timu hizi mbili.
    Ukirudi kwa historia kidogo hizi timu zilianza hata kabla Taifa letu la Tanzania halijapata kuwa huru na naweza kusema kuwa moja ya msukumo wa kuanzisha hivi vilabu ilikuwa ni kuwaunganisha watanganyika kipindi hicho kwa lengo la kupata nafasi ya kujadili mambo mbalimbali yanayohusiana na ukombozi wa Taifa hili ndio mana sishangai kuona Mzee Karume akitajwa kuwa sehemu muhimu ya upatikanaji wa majengo ya klabu mbili hizi kwa maana ya jengo la Jangwani kwa upande wa Yanga SC na lile la Msimbazi kwa upande wa Simba SC kwani ukaribu wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Aman Karume ulichochea haya na baada kuja kuzaa Tanzania ambayo ni muunganiko wa Tanganyika na Zanzibar.
    Ni zaidi ya miaka 80 sasa timu hizi kubwa zipo vilevile zaidi kinachoongezeka ni idadi ya mashabiki tu na ule utani wa jadi lakini kwenye mali nyingine za klabu mambo ni yaleyale.
    Uko nyuma kidogo walijitokeza watu ambao tuliwahita wafadhili watu hawa walika maarufu sana sana walisajili wachezaji walitoa posho,mishahara na kununua jezi,kanga,vitambaa na vitu vidogovidogo vya hamasa na watu walifurahi sana na kama walifanya chochote kwenye yale majengo mawili basi itakua walipaka rangi yale majengo na baada ya hapo walivuna umaarufu na pesa kibao kupitia timu hizi na kisha wakaenda zao na kuziacha hizi timu palepale yani ni sawa unakaa na ndugu ambaye hataki kukutafutia kazi ila anakuhudumia wewe,watoto wako na mke wako kwa kila mkitakacho ila hayupo tayari wewe upate kazi au ufungue biashara yako,kama upo vizuri kichwani lazima ujihoji kwa hili.
    Ilifika hatua walijenga hofu kwa watu hasa wadau wa michezo na kuamini kuwa hizi timu haziwezi kufanya lolote bila watu wale wajanja na kila walipotokea watu wachache kuhoji chochote kuhusu muenendo wowote juu ya wafadhili hawa kundi kubwa la watu ambao ni sawa na wale wanatengemea msaada wa ndugu yule msaidiaji walikuja juu na kutoa matamko mazito na kuwaita watu wale wasaliti na mamluki ambao wametumwa kuwafitinisha na mfadhili wao jambo ambalo lilifanya vilabu hivi kubaki palepale hata leo tunasimama hapa havina lolote la kujivunia zaidi ya yale maono ya mwanzo na bahati vilijengwa eneo ambalo mji ndio umeshamili vingejengwa uko vikindu aisee saivi yangekua magofu makazi ya popo.
    Wimbi la wafadhili likaenda na kufikia tamati na walewale wafadhili wajanja wachache wakajigeuza na kuja na wazo la kutaka hizi timu ziwe kampuni swala la kuendeshwa na wanachama halina tija tena na kutaka ziwe kampuni lakini wakati uho wao wamefaidika mara mia zaidi kuliko timu zenyewe na wamekua wakubwa kuliko hizo timu na kunifanya nikumbuke ule ujanja uliokuwa unatumika na baadhi ya wafanya biasha hapa nchini kwa kubadilisha majina ya hotel kubwa flani na kujifanya wawekezaji wapya.
    Mabadiliko hayo yalileta mvurugano na hata wale waliokubali hawakujua kwanini wanakubali na hata waliokataa nao hawakujua kwanini wanakataa aliyejua maana alibaki kuwa ni yule mwenye agenda yake tu.
    Mambo yakaenda vurugu zikashamiri na hatimaye upepo ukabadilika na kuamia kwenye uwekezaji ambapo sasa ni habari ya mjini na kila upande umekuwa ukihaha kuhakikisha unaingia uko kwenye uwekezaji ingawa bado hofu yangu walewale walionza toka ufadhili ndio wapo na agenda zao ni zilezile kwa sura mpya tena ya kitoto na kazi inakua rahisi kwani badala ya kutumia kiswahili unaweka kizungu tena kwenye maandishi na unapata wajanja wachache wajukuu wa  bibi basi kazi inakuwa rahisi.
    Kuwekeza si kitu kibaya endapo uwekezaji uho utakuwa na manufaa kwa pande zote na mfumo ulio rasmi kwa soka letu ni ule ambao tumeutoa nchini Ujerumani ambao katika asilimia 100 basi asilimia 51 ubaki kwa wanachama na zile 49 kwenda kwa wawekezaji na sio muwekezaji ikiwa na maana kuwa ni lazima waanzie watu watatu na kuendela ili kuzigawa zile asilimia 49 kulingana na uwezo wao wa kumiliki shea na lengo kuu hasa la huu muundo ni kuzuia uwezekano wa mtu mmoja kua na nguvu ya kimaamuzi kwenye vikao vya bodi ambavyo vitakwenda kuamua mambo mbalimbali ya klabu husika kufanya kuwe na mlingano wa hoja na kulinda maslahi ya klabu husika.
    Ni mfumo ambao umekuwa ukitumika vema nchini ujerumani na vilabu kama bayani munichi vimefanikiwa kuwa vilabu tajiri ulaya na duniani kote kutokana na mfumo huu.
    Kwa mtazomo wangu ni kuwa tunapoamua kufanya uwekezaji basi tufanye kweli milango iwe wazi na sio kuja kwenye mfumo huu tayari tunajina letu mfukoni makundi yanatoka wapi?kwanini tunabisha?malumbano yanakujaje?kwani huyo asemwe na wengine wakingie kifua?hawa wanao sema na wanaopinga nani yupo sahahi? wote nyie si wajukuu wa bibi?tatizo nini?
    Ukijiuliza maswali hayo utagundua kitu kuwa bado hatuko na dhamira ya dhati kuzikomboa klabu hizi bado kuna ujanja wa wajukuu wachache pengine wao kidogo walitoa ujinga kwa kupata shule na kutaka kutumia shule zao kuumiza wengine.uwazi mbona haupo?mbona hoja ngumu ujibiwa kwa majibu mepesi?hivi viburi na dharau vinatoka wapi ni hili hili shamba la bibi?
    Ifike mahali nyie wajanja wachache msitutoe akili dunia imebadilika sana hata sisi wa uku shamba tumepata elimu kidogo tunauelewa jamani wa haya mambo msifunike funike mambo kama kweli mnalenga au mnamaanisha  uwekezaji   kwa manufaa ya timu zetu basi kuweni wazi wadau wanatamani kuona vilabu hivi vinakua sio kwa idadi ya mashabiki tu hapana hata hali za kiuchumi ziboreke pia.
    kwa idadi ya mashabiki, wapenzi na wanachama wa vilabu hivi walivyo wengi kukiwa na mipango thabiti na yenye maslahi mapana ya klabu hizi hakuna shaka vitakuwa ni miongoni mwa vilabu tajiri barani Afrika na sio kuwawekea watu hofu na kuamini kuwa bila ya watu fulani vilabu hivi haviwezi kwenda jambo ambalo si kweli kabisa..
    Pia tukumbuke kuwa hivi vilabu vipo Dar es salaam lakini vina mashabiki nchi nzima na wanashiriki kwa namna moja au nyingine kuona vilabu vinasonga mbele hivyo ni vema nao kuwashirikisha.
    Tunahitaji uwekezaji wenye tija tujenge mazingira rafiki ili hata watu wenye nia njema na maendeleo ya mpira wetu wavutike lakini pia hata vilabu vingine vione mwanga na kujifunza kupitia ninyi.
    Tusitumie vibaya uelewa wa kawaida wa walio wengi kupeleka mambo visivyo ili tu kutengeneza mazingira ya maslahi binafsi ila tutengeneze mambo ya maana ili taifa lisonge mbele hasa kupitia soka.
    Natamani kuendelea sans ila mambo ni mengi pia kwa leo tuishie hapa.

    (Dominick Salamba ni mchambuzi wa michezo, pia anapatikana katika Instagram akaunti kupitia @dominicksalamba au waweza kuwasiliana naye kwa namba +255 713 942 770)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UWEKEZAJI KATIKA KLABU TANZANIA UMEGUBIKWA NA SINTOFAHAMU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top