• HABARI MPYA

    Monday, July 15, 2019

    SINGANO ‘MESSI’ KUJIUNGA NA MAZEMBE BAADA YA MICHUANO YA KOMBE LA KAGAME

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIUNGO mshambuliaji mpya wa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Ramadhani Yahya Singano ‘Messi’ atajiunga na timu baada ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
    Messi, mchezaji wa zamani wa Simba SC amejiunga na Mazembe kwa kusiani mkataba wa miaka mitano akitokea Azam FC kama mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake.
    Anakuwa Mtanzania wa pili kusajiliwa majira haya baada ya mshambuliaji, Eloius Ambokile kutoka Mbeya City.
    Ramadhani Singano ‘Messi’ atajiunga na TP Mazembe baada ya michuano ya Kombe la Kagame inayoendelea mjini Kigali, Rwanda

    Wawili hao wanatarajiwa kwenda kukumbushia enzi za Watanzania wengine wawili, winga Thomas Ulimwengu na mshambuliaji Mbwana Ally Samatta waliong’ara mwanzoni mwa muongo huu hadi katikati kabla ya wote kuondoka awamu wakifuatana ndani ya miaka miwili.
    Mazembe pia imemsajili Lamisha Musonda mwenye umri wa miaka 27, mchezaji wa zamani wa Anderlecht, Chelsea, Mechelen, Llagostera na Palamos ya Hispania ambaye amepewa nafasi ya kujiinua upya.
    Wawili hao waliitumikia Mazembe kwa mafanikio kuanzia mwaka 2011 kabla ya wote kuondoka wakifuatana, Samatta akianza 2016 kujiunga na KRC Genk ya Ubelgiji na Ulimwengu akifuatia 2017 kujiunga na AFC Eskilstuna ya Sweden kabla ya kuhamia, FK Sloboda Tuzla ya Bosnia, Al-Hilal ya Sudan mwaka 2018 na sasa JS Saoura ya Algeria.
    Kwa sasa kikosi cha Mazembe kipo mjini Kigali nchini Rwanda ambako kesho kitamenyana na mabingwa watetezi, Azam FC katika Robo Fainali ya Kombe la Kagame Uwanja wa Nyamirambo.
    Robo Fainali nyingine itafanyika kesho pia kati ya KCCA ya Uganda na wenyeji, Rayon Sports kabla ya Jumatano wenyeji wengine APR kumenyana na Manyema Union na Gor Mahia ya Kenya dhidi ya Green Eagles ya Zambia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SINGANO ‘MESSI’ KUJIUNGA NA MAZEMBE BAADA YA MICHUANO YA KOMBE LA KAGAME Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top