• HABARI MPYA

    Saturday, July 20, 2019

    SIMBA SC KUCHEZA MECHI YA KWANZA YA KUJIPIMA NGUVU JUMANNE AFRIKA KUSINI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM  
    KLABU ya Simba SC Jumanne itacheza mechi yake ya kwanza ya kujipima nguvu katika kambi ya Afrika Kusini kujiandaa na msimu mpya itakapomenyana na timu ya Chuo Kikuu cha Orbit Tvet mjini Rusternburg.
    Simba SC imetoa orodha ya mechi nne za kujipima nguvu leo ikianza na timu hiyo ya Ridhaa inayoshiriki Ligi za chini Afrika Kusini Jumanne.
    Mechi nyingine ni dhidi ya Platinums Stars ya Rusternburg Jumatano, Township Rollers ya Botswana Julai 27 na Orlando Pirates ya Johannesburg Julai 30 zote za Ligi Kuu ya nchini humo.
    Baada ya kusajili wachezaji wazuri kuboresha kikosi chake, mabingwa hao wa Tazania Bara wapo Afrika Kusini kwa maandalizi ya msimu mpya. 




    Simba SC Jumanne itamenyana na Orbit Tvet mjini Rusternburg 

    Simba SC imesajili wachezaji 11 wapya, ambao ni kipa Beno David Kakolanya, baki Gardiel Michael Mbaga na kiungo Ibrahim Ajibu Migomba wote kutoka Yanga SC, ambao kwa pamoja na beki wa kati, Kennedy Wilson Juma kutoka Singida United na Miraj Athumani ‘Madenge’ kutoka Lipuli wanafanya idadi ya wachezaji watano wazawa wapya Msimbazi hadi sasa.
    Wengine sita wote ni wa kigeni, Wabrazil mabeki beki Gerson Fraga Vieira ATK ya Ligi Kuu ya India na Tairone Santos da Silva kutoka klabu ya Atletico Cearense FC, mshambuliaji, Wilker Henrique da Silva kutoka Bragantino, zote za Daraja la Nne nchini Brazil na viungo Mkenya, Francis Kahata Nyambura, Msudan Sharaf Eldin Shiboub Ali Abdalrahman na winga Deo Kanda kutoka TP Mazembe ya kwao, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Pamoja na kusaini wachezaji wapya, Simba SC pia imewapa mikataba mipya wachezaji wake kadhaa wa msimu uliopita, wakiwemo kipa Aishi Manula, mabeki Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, Nahodha Msaidizi, Mohammed Hussein ‘Tshabalala, Muivory Coast, Serge Wawa Pascal viungo Jonas Mkude, Mzambia Clatous Chama na washambuliaji Nahodha Mkuu, John Bocco na Meddie Kagere raia wa Rwanda.
    Miongoni mwa wachezaji watakosekana Simba SC ni pamoja na Waganda, beki Juuko Murshid na mshambuliaji Emmanuel Okwi ambao wote wanaondoka.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC KUCHEZA MECHI YA KWANZA YA KUJIPIMA NGUVU JUMANNE AFRIKA KUSINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top