• HABARI MPYA

    Tuesday, July 09, 2019

    RAIS WA TFF, KARIA ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI MSIBA WA WAFANYAKAZI AZAM TV

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia ametuma salamu za rambirambi kwa Mkurugenzi wa Azam Media, familia, ndugu, jamaa na marafiki wa wafanyakazi wa Kituo cha Azam TV waliopoteza maisha kwenye ajali ya Gari jana.
    Katika salamu hizo za rambirambi Rais wa TFF, Karia amesema ni mshtuko mkubwa kupokea taarifa ya Wafanyakazi hao wa Azam Tv kupoteza maisha.
    Kwa niaba ya TFF Rais Karia ametoa pole kwa Mkurugenzi wa Azam Media ambako walikua wanafanya kazi, familia, ndugu, jamaa na marafiki.
    Amewataka kuwa na subira katika kipindi hiki kigumu cha kuwapoteza wapendwa wao.

    Watu saba wakiwemo wafayakazi watano wa Azam TV walifariki dunia katika ajali jana eneo la Shelui, Singida baada ya gari mbilikugongana uso kwa uso.
    Wafanyakazi hao wa Azam TV walikuwa njiani kwenda kurusha matangazo mbashara ya uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato.
    Wafanyakazi wa Azam TV waliofariki kwenye ajali hiyo ni Salim Mhando (muongozaji wa matangazo), Florence Ndibalema (Mhandisi wa Sauti), Sylvanus Kasongo (Mhandisi Mitambo) na wapiga picha wawili Said Haji na Charles Wandwi.
    Watu wengine wawili waliofariki ni dereva wa gari ambalo Azam TV walilikodi pamoja na msaidizi wake, majina ya wawili hao bado hayajapatikana.
    Wafanyakazi watatu wa Azam TV wamejeruhiwa ambao ni Artus Masawe, Mohammed Mwinshehe na Mohammed Mainde. Mungu azilaze roho za marehemu mahala pema peponi, Amina.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAIS WA TFF, KARIA ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI MSIBA WA WAFANYAKAZI AZAM TV Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top