• HABARI MPYA

    Thursday, July 11, 2019

    AFCON ISIWE CHANZO CHA HISTORIA YA MAUMIVU KATIKA SOKA YETU

    Na Dominick Salamba, DAR ES SALAAM 
    WASWAHILI wana misemo sana nimekumbuka msemo mmoja unaosema kuwa kila mtu ana zamani zake,wakiwa na maana kuwa hata mimi pia nina zama zangu za kujidai,jambo linalo nipelekea nikumbuke stori za zama zangu kutoka kwenye kitabu cha hadithi za kuchekesha na kufikirisha kitabu cha Abunuwasi.
    Ambapo moja ya visa vyake ni  hiki' Abunuasi alijenga nyumba yake ya ghorofa 4 ambapo alipanga afanye biashara zake ili atengeneze faida na kukua kiuchumi,alifanikiwa kuzimaliza na kufanya biashara zake ambazo hazikuleta matunda chanya hivyo akaamua kubadili mawazo na kuamua kutangaza kuziuza nyumba zile za juu kwa maana aliuza ghorofa ya 1,2,3 na 4  na yeye kubakiwa na ile nyumba ya chini ambapo aliishi mwenyewe na wanunuzi wa juu waliendelea na maisha yao bila shaka lakini hata baada ya kuuza zile nyumba na kudhani labda atapata afueni ya maisha lakini bado haikua kama alivyowaza na kila alipowaona wanunuzi wa zile nyumba za juu aliwaona wakiwa na furaha na maisha kuwaendea vema jambo ambalo lilimchanganya kama si kumkera na kuamua kubadili mawazo na kuona ni vema arudi kijijini alipozaliwa hivyo alileta gari na kupakia mizigo yake na kuleta greda au tingatinga na kuchukua kibaza sauti na kuwatangazia wanunuzi wake wa juu kuwa yeye ana hama pale chini hivyo anataka kubomoa nyumba yake ili aondoke kwahiyo anawaomba kila mmoja aishikilie nyumba yake uko juu wakati yeye anabomoa yake wasije mlaumu. Unajua nini kilifuata? 
    Tuachane na stori ya Abunuasi turudi kwenye mada yetu kama tunavyojua huu mwaka 2019 umekua mwaka mkubwa na wenye historia kwa upande wa soka kwani tumeshiriki michuano mikubwa barani afrika baada ya kusubiri kwa takribani miaka 39 hivyo sio kitu kidogo kwa bara lenye zaidi ya nchi 53 na sisi kuwa miongoni mwa mataifa 24 ambayo yalishinda na kuingia katika Fainali zinazoendelea uku nchini Misri kwa hatua ya robo fainali..
    Sio kwa kwa miaka yote hiyo 39 hatukupambana au hatukua na mikakati hapana tulipambana kwa namna mbalimbali ila huu mwaka imewezekana na timu imekwenda imetoka katika hatua ya makundi kwa kucheza michezo 3,na kupoteza yote 3 na kufunga mabao 2 uku ikifungwa mabao 8 na mataifa ya Senegal 2-0,Kenya 3-2 na Algeria 3-0.ukingalia unaweza kudhani kama tumefanya vibaya sana ila kuna msemo unaosema unapomuona mtu anakimbia sana basi si vibaya kumsifia na yule anae mkimbiza,
    Hulka ya binadamu ni kutamani vitu vipya na vizuri kadri anavyozidi kupata anavyovihitaji kiu yetu kubwa ilikua walao kufudhu Fainal hizi jambo ambalo tumefanikiwa na mara baada ya kufanikiwa yakatokea malengo mengine makubwa na ya gafla kua tunaenda kushinda yani tukawafunge Senegal,Kenya na Algeria kwa sababu nyepesi kabisa kua wao watacheza 11 kama sisi,mpira unadunda,hamasa kubwa pamoja na sara za kutosha za watanzania zaid ya milioni 55.Si vibaya kuwaza mambo mazuri na kuwatia moyo wapambanaji wetu na ni jambo jema ila kilichonishangaza ni baada ya kupoteza tukaanza kujawa na hasira na kuona kuna watu wametudhurumu,hawakuwajibika na kuona wao ndio sababu za kufanya vibaya hivi ni kweli au tunaongea ili tuonesha uhodari wa kujenga hoja?
    Hata kabla ya timu kurudi nchini tayari tayari maoni mbalimbali yalitoka juu ya mwenendo wa timu na kuchagizwa na kitendo cha Uganda,Misri,Morocco na wengine ambao wameachana na waalimu wao bila hata kujua makubaliano na sababu ambazo wao zimewafanya waachane na waalimu wao kwani naamini mipango ya Uganda kisoka na hao wengine ni tofauti ya yetu na kuumbuka ule msemo wa sio kila anae acha mke basi ujue alimfumania mkewe wengine wameacha wake kwa kuwa tu wake zao hawajui kupika.
    Baada ya Timu kurejea tulisikia mengi ikiwa pamoja na kamati ya amasha kuishukuru timu ikiwa pamoja na kuwaomba watanzia kuinga mkono timu kuelekea kufuzu michuano ya CHAN ambao Tanzania itacheza na Kenya mara zikazagaa taarifa za kusitishwa kazi kwa mwalimu wa timu ya Taifa gafla likatoka tamko la waziri mwenye dhamana na michezo kukanusha na kudai kua mwalimu yupo sana kabla kauli haijakolea chumvi wenye mpira wao TFF wakatangaza kumfuta kazi mwalimu huyo na kusema wapo mbioni kumtangaza mwalimu wa mda atakae ongoza kikosi hicho kuelekea kufuzu michuano ya CHAN na hapo ndipo tatizo likazidi kukolea mara baada ya waziri mwenye dhamana kuwaita viongozi wa Tff na kutaka waende na ripoti ya mashindano yaliyopita lakini pia waende na mkakati wa timu ya Taifa katika mashindano yajayo na siku ya mkutano viongozi wa mpira hao hawakutokea na kuzua sintofahamu na wengine kutafsiri kua wametunisha msuli kwa waziri mwenye dhamana.

    Lakini bado waziri hakuchoka na kupanga tarehe nyingine na kutamka kua mkutano uho wa pili utakua wa wazi wadau,waandishi na mwalimu aliyesitishiwa mkataba awepo na mambo yataongelewa kwa uwazi kwani jukumu la timu ya Taifa lipo mikononi mwa serikali kupitia wizara husika..
    Wote tunajua serikali ndio msimamizi wa kila kitu nchini Tanzania na kupitia wizara ya michezo ambapo kuna baraza la michezo Taifa hawa ndio watunga sera na wasimamizi na washauri wa karibu wa vyama mbalimbali vya michezo ikiwemo TFF ingawa Tff inawajibika kwa FIFA na sera ya FIFA ni kutotaka serikali za mataifa wanachama kutoingilia shughuli za uendeshwaji wa soka na kama ikibainika kuwa kuna misuguano hiyo na kushindwa kupatiwa ufumbuzi ina maana nchi husika itafungiwa uanachama mpaka pale FIFA watakapo jiridhisha kuwa mambo yapo sawa.
    Na madhara yatakayo tokea baada ya nchi kufungiwa ni makubwa sana kwani ukifungiwa na Fifa ina maana na Caf nao wanakufungia kwahiyo hatutaweza kushiriki michuano yeyote inayoandaliwa na mashirikisho haya iwe timu ya Taifa au vilabu vyetu kama ndivyo basi hata ligi yetu itakosa maana uku tukijua kua vilabu vyetu vimesajili wachezaji mbalimbali kutoka pande zote za dunia hivyo gharama na mambo mengine mengi yatakua ni hasara kubwa kwa vilabu,Lakini pia kuna misaada mbalimbali kutoka Fifa na Caf katika kuendeleza soka kwa maana vijana na mafunzo mbalimbali ya utawala,masoko waalimu vyote vitakoma na kuturudisha nyuma hatua 100.
    Wito wangu kabla hatujaangalia ufahari wetu,maslahi yetu,jeuri zetu tuangalie zaidi maslahi mapana ya Taifa letu pendwa sisi bado ni wachanga kisoka viongozi wa TFF na serikali kupitia Wizara husika wekeni chini tofauti zenu simameni kwenye weledi na uzalendo mfikie muafaka na kuepusha mabalaa ambayo hayana sababu kama ambavyo TFF mlibariki BMT kusimamia mchakato  wa uchaguzi wa moja ya klabu kubwa hapa nchini ndivyo mkubali kupokea ushauri na maelekezo ya Serikali kupitia wizara kwani wizara ina wataalamu mbalimbali na ndiyo mhimili wa michezo yote hapa nchini sio soka tu soka ni sehemu tu msijisahau mkaona mnaishi juu hapana mpo juu ila chini anaishi Abunuwasi ambaye akiamua kuondoka basi itawalazimu kuzishikia nyumba zenu na kuumiza wengi.
    Hatua tuliyofika si ndogo ilitaka tu muendelezo tumeona uganda walipoingia mwaka 2017 hawakushinda mchezo wowote ila mwaka 2019 wameshinda mchezo 1 sare 1, na kupoteza 1 na kutinga hatua 16 bora kwani maendeleo ni hatua na si vinginevyo.Kinyume ha hapo tutazikumbuka fainal hizi kwa machungu ambayo mnataka kuyaleta naamini bado mda upo na mtatengeneza mambo ili tuone tukipiga hatua na msisahau kua hakuna njia ya mkato ni lazima tuanzie chini na chini yenye mwendelezo.
    Ebwana jamaa yangu wa kahawa ndio anapita hapa kijiweni leo hata mazoezi siendi ni mwendo wa kahawa na kashata.

    (Dominick Salamba ni mchambuzi wa michezo pia anapatikana kwa simu namba +255 713 942 770 na unaweza kumfollow Instagram  @dominicksalamba)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AFCON ISIWE CHANZO CHA HISTORIA YA MAUMIVU KATIKA SOKA YETU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top