• HABARI MPYA

    Tuesday, July 23, 2019

    SIMBA SC YAANZA VYEMA MECHI ZA KIRAFIKI AFRIKA KUSINI, YAIPIGA ORBIT TVET 4-0 RUSTERBURG

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Simba SC leo imeanza vyema mechi zake za kujipima nguvu katika kambi ya Afrika Kusini kujiandaa na msimu mpya nchini Afrika Kusini baada ya kuichaoa mabao 4-0 timu ya Chuo Kikuu cha Orbit Tvet mjini Rusternburg.
    Mabao ya Simba SC yamefungwa na Nahodha na mshambuliaji tegemeo, John Raphael Bocco dakika ya tisa na 28, kiungo Hassan Dilunga dakika ya 23 na mshambuliaji mpya, Wilker Henrique da Silva kutoka Bragantino ya Daraja la Nne kwao, Brazil dakika ya 30.
    Baada ya mchezo wa leo, Simba itateremka tena uwanjani kesho kumenyana na Platinums Stars ya Rusternburg, Township Rollers ya Botswana Jumamosi na Orlando Pirates ya Johannesburg Julai 30.
    Simba SC imeweka kambi mjini Rusterburg, Afrika Kusini kujiandaa na msimu mpya na itaanza na Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kumenyana UD do Songo ya Msumbiji katika Raundi ya kwanza.
    Mabingwa hao wa Tanzania Bara wataanzia ugenini kati ya Agosti 9 na 11 kabla ya kurejea nyumbani kwa mchezo wa marudiano kati ya Agosti 23 na 25.
    Ikifanikiwa kuvuka raundi ya kwanza, Simba itakutana na mshindi kati ya FC Platinum ya Zimbabwe na Nyasa Bullets ya Malawi na ikifuzu mtihani huo pia itaingia tena hatua ya makundi.
    Ratiba hii ya Ligi ya Mabingwa Afrika itailazimisha Simba SC kupanga tarehe nyingine ya tamasha lake la kila mwaka la kutambulisha kikosi kipya, Simba Day ambalo hufanyika Agosti 8, kwa sababu siku hiyo watakuwa Msumbiji kwa ajili ya mechi na UD do Songo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAANZA VYEMA MECHI ZA KIRAFIKI AFRIKA KUSINI, YAIPIGA ORBIT TVET 4-0 RUSTERBURG Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top