• HABARI MPYA

    Sunday, July 28, 2013

    KIM POULSEN AMWAGA MBIVU NA MBICHI KIPIGO CHA STARS JANA, ASEMA NI FEDHEHA KUBWA NA HANA HAMU

    Na Mahmoud Zubeiry, Kampala, IMEWEKWA JULAI 28, 2013 SAA 2:35 ASUBUHI
    KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mdenmark Kim Poulsen amesema kwamba imemsikitisha sana kutolewa kwenye michuano ya Ubingwa wa Mataifa wa Afrika (CHAN), inayohusisha wachezaji wanaocheza Ligi za nchini mwao pekee, lakini sasa anajipanga upya kurejesha makali ya timu.
    Bao la kwanza; Hivi ndivyo Stars ilivuofungwa bao kwa kwanza

    Stars imefungwa mabao 3-1 jana na Uganda Uwanja wa Mandela, Namboole mjini hapa na kufanya kipigo cha jumla cha 4-1 baada ya awali kufungwa 1-0 Dar es Salaam na kuwapa The Cranes, Korongo wa Kampala, tiketi ya kwenda Afrika Kusini kwenye CHAN mwakani.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana baada ya mechi, Poulsen alisema kwamba kutolewa CHAN si mwisho na wamejifunza kutokana na makosa, yeye pamoja na wachezaji wake- na sasa wanajipanga upya kuendelea na safari.
    Amechoka; Kocha Poulsen
    amesema kipigo cha jana
    kimemsononeshs sana

    “Mimi na wachezaji tumesikitishwa kutolewa kwenye CHAN, ulikuwa mchezo mgumu nimesikitishwa, tumeanza kinyonge, baada ya dakika 10 tukafungwa 1-0, baada ya hapo nafikiri tumeona tulijiandaa vizuri kwa huu mchezo, tulianza kucheza vizuri, tukafunga ikawa 1-1,”.
    “Na Ngassa akagongesha mwamba kwa shuti la ajabu na kabla ya mapumziko, Frank Domayo akaumia. Na hii ilikuwa pigo kwa timu kwa sababu huu umekuwa muendelezo wa mwezi mgumu kwetu, tunakosa wachezaji fulani, na sasa ikatubidi tumkose mwingine mmoja,”.
    “Lakini pamoja na yote, kipindi cha pili tulimiliki vizuri mpira, tulihitaji bao moja tufuzu, lakini baada ya hapo, likaja pigo tena kwetu, ndani ya boksi kukiwa hakuna mtu, tukawapa wao penalti (David Luhende alinawa akiwa peke yake). Na unapofanya kosa kubwa kama hili, unajitengenezea ugumu,”.
    “Tukiwa nyuma kwa mabao 2-1, tukapata kona, wakaokoa kwenye mstari, ingekuwa 2-2. Na katika shambulizi hilo hilo, tukapoteza mpira kwa kosa kubwa, na wakafanya shambulizi la kushitukiza tukafungwa, ikawa 3-1,”.
    “Pia nikashangazwa sana, baada ya mchezo kuwa sisi tumefungwa 3-1, kisha marefa ndiyo wakabadilika na kuwa wazuri kwa Tanzania. Lakini kabla ya hapo, kila tukio la asilimia hamsini kwa hamsini, walipewa wenzetu. Hivyo nafikiri marefa walikuwa wachanga, ambao hawajakomaa kiasi cha kuumudu mchezo kama huu,”.
    Alipoulizwa kuhusu ahadi yake ya kuipeleka Stars fainali zijazo za Mataifa ya Afrika (AFCON) baada ya kuanza kazi Mei mwaka jana, Poulsen alisema kwamba amesikitishwa na kutolewa CHAN, lakini wanatakiwa kusimama imara na kuendelea na mapambano.
    “Tumekuwa katika kazi hii kwa miezi 14, mwanzoni tumecheza vizuri sana, hii ni mara ya kwanza ninaangushwa, kuangushwa haswa leo, lakini wakati huo huo, katika soka unatakiwa kuwa imara, kama unataka kushinda kila mchezo, ucheze vizuri, tumepoteza mchezo ambao tayari tulijitengenezea mazingira magumu katika mchezo wa kwanza Dar es Salaam. Mimi ni aina ya watu hawa, na wachezaji ni wa aina hiyo pia, ukipoteza mechi, unajifundisha kutokana na makosa, kisha unasonga mbele,”.
    “Tuna malengo yetu, tunatakiwa kujizatiti, tunaweza kujizatiti na kusonga mbele, tunaweza kufanya na tutafanya. Nilikuambia, unapoanza safari inakuwa na kona, kunakuwa na vigingi barabarani. Hivi vilikuwa vigingi na kona. Ni pigo, tumesononeshwa kuwa nje ya CHAN, lakini si mwisho, tuko tayari kupambana upya,”alisema.
    Jana alikuwepo uwanjani; Ngassa
    akijiandaa kupiga krosi iliyozaa
    bao la Stars jana

    Ndoto za Stars kucheza Fainali za pili za CHAN baada ya mwaka 2009, jana zilizimika kufuatia kufungwa na Uganda mabao 3-1 na kutolewa kwa jumla ya mabao 4-1, baada ya wiki mbili zilizopita kufungwa 1-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Shujaa wa Korongo la Kampala inayofundishwa na Mserbia, Milutin Sredojevic ‘Micho’ jana alikuwa ni Frank Kalanda anayechezea Timu ya Mamlaka ya Mapato (URA) ya hapa aliyefunga mabao mawili. 
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Kanoso Abdoul Ohabee, aliyesaidiwa na Andirvoavonjy Pierre Jean Eric na Jinoro Velomanana Ferdinand wote kutoka Madagascar, hadi mapumziko timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1.
    Uganda walianza mchezo kwa kasi ndani ya dakika 10 za mwanzo walilitia sana misukosuko lango la Stars na hatimaye wakafanikiwa kupata bao dakika ya saba, mfungaji Frank Kalanda, baada ya kutokea kizazaa langoni mwa Stars.
    Hata hivyo, baada ya bao hilo, mabeki wa Stars walilaumiana kidogo na kipa wao kwa kosa lililoruhusu bao, lakini wakazinduka na kuanza kucheza vizuri.
    Stars ilianza kushambulia kwa kutumia mipira mirefu ya pembeni iliyokuwa ikipelekwa kwa Mrisho Ngassa na kwa mtindo huo, ilifanikiwa kupata bao la kusawazisha dakika ya 14.
    Ngassa alipokea mpira mrefu wa Athumani Iddi ‘Chuji’ upande wa kushoto mwa Uwanja, akamtoka beki wa Uganda Nicolas Wadada na kutia krosi maridadi iliyowapita mabeki wa kati wa Cranes na kumkuta Amri Kiemba aliyefumua shuti zuri mpira ukatinga nyavuni.
    Baada ya bao hilo, Uganda walipoteana na Stars ikaanza kutawala mchezo, ingawa haikufanikiwa kupata bao. Dakika ya 43, Stars ilipata pigo baada ya kiungo wake, Frank Domayo kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Simon Msuva.
    Kipindi cha pili Stars walikianza vizuri, dakika mbili za mwanzo, lakini kosa moja tu la beki David Luhende kuunawa mpira kwenye eneo la hatari, akiwa peke yake liliwapa penalti wenyeji na Brian Majwega akaenda kumtungua vizuri Juma Kaseja dakika ya 48.
    Stars ilizinduka tena na kuanza kushambulia lango la Uganda, ingawa na wenyeji nao waliendelea kushambulia.  
    Hata hivyo, kosa la Salum Abubakar ‘Sure Boy’ katika dakika ya 62 liliipa Uganda bao la tatu. Stars walipata kona, ilipopigwa ikaokolewa na mpira ukamkuta Kiemba, lakini wakati Simon Msuva na Ngassa wamefungua pembeni, kiungo huyo akataka kupiga chenga katikati ya watu wawili.
    Akapokonywa mpira na Hassan Waswa wakati huo wachezaji wote wa Stars wamepanda kwa ajili ya kona, Brian Majwega akafungua kushoto. Waswa akamvuta beki pekee wa Stars aliyekuwa amebaki nyuma, Kevin Yondan akapeleka pasi kwa Majwega, akatia krosi Kalanda akamtungua Kaseja.
    Mchezo ulikuwa wa Uganda tangu hapo, Stars wakicheza kwa presha ya kutoruhusu mabao zaidi na wakati huo huo wakisaka mabao, jambo ambalo liliwapa kazi nyepesi wenyeji kuutawala mchezo.
    Stars inatolewa kwenye CHAN ikiwa tayari imepoteza matumani ya kufuzu kwenye Fainali za Kombe la Dunia mwakani katika Kundi lake, D baada ya kufungwa mechi mbili mfululizo nyumbani na ugenini, 2-1 dhidi ya Morocco mjini Marakech na 4-2 dhidi ya Ivory Coast Dar es Salaam mwezi huu. 
    Siyo mwisho wa maisha; Pamoja na kutolewa CHAN na Kombe la Dunia, bado kuna mashindano mengine mbele, ikiwemo mechi za kufuzu AFCON

    Aidha, huu unakuwa mchezo wa nne mfululizo Tanzania inafungwa- mbili ugenini wa leo na wa Morocco 2-1, Ivory na Coast na Uganda wiki mbili zilizopita. Ikiwa ina mechi moja ya kukamilisha Ratiba katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia mwakani nchini Brazil dhidi ya Gambia, Stars inatakiwa kujipanga kwa ajili ya mechi za kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika zinazotarajiwa kuazna mwishoni mwa mwaka huu.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: KIM POULSEN AMWAGA MBIVU NA MBICHI KIPIGO CHA STARS JANA, ASEMA NI FEDHEHA KUBWA NA HANA HAMU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top