• HABARI MPYA

    Thursday, July 25, 2013

    BONGE LA BEKI LAOTA MBAWA SIMBA SC, MSIMBAZI SASA...

    Na Prince Akbar, IMEWEKWA JULAI 25, 2013 SAA 6:15 MCHANA
    RAYON Sport ya Rwanda imeikatili ile mbaya Simba SC, baada ya kumuongezea Mkataba, beki wake mahiri wa kati, Faustine Usengimana hivyo kuzima ndoto za Wekundu wa Msimbazi kumpata mlinzi huyo hodari anayeinukia vizuri.
    BIN ZUBEIRY inafahamu Usengimana amesaini Mkataba mpya wa miaka miwili na mabingwa hao wa zamani wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame na sasa Simba SC hawatampata.
    Bonge la beki; Fausitine Usengimana ameamua kubaki Rwanda na kukataa kuja Tanzania kuchezea Simba SC

    Tayari Simba SC wana taarifa za Usengimana kuamua kubaki Rwanda na wamehamishia mawindo yao kwa beki wao wa zamani, Mganda Joseph Owino ambaye kwa sasa anachezea URA ya kwao.
    Pamoja na beki huyo, Simba SC imeshauriwa na mshambuliaji wao mpya, Mrundi Amisi Tambwe isajili beki mwingine hodari Mrundi na imekwishaanza mipango hiyo. 
    Kumbuka Simba SC imeachana na mabeki wote waliokuwa majaribioni, Waganda Assumani Buyinzi na Samuel Ssenkoom na inataka ukuta wake uundwe na Owino na beki kutoka Burundi. 
    Simba SC pia imemtema kiungo Mganda, Mussa Musse na kwa maana hiyo mchezaji wa kigeni iliyenaye sasa ni mmoja tu, kipa Mganda, Abbel Dhaira.
    Dhaira anaweza kuungana na Waganda wenzake wawili, Owino na Moses Oloya walio katika mpango wa kusajiliwa SImba SC wakati wachezaji wengine watakaokamilisha idadi ya wachezaji watano wa kigeni ni Warundi, Tambwe na mwenzake.
    Pamoja na hayo, baadhi ya wapenzi wa klabu hiyo wameendelea ‘kumchanganya’ kocha Alhaj Abdallah Athumani Seif ‘King Kibaden’ kwa kumletea wachezaji wa kuwajaribu.
    Mpenzi mmoja ameleta beki kutoka klabu ya Black Leopard ya Afrika Kusini, Vincent Matsobane Mabusela na mwingine anataka kuleta beki kutoka Ghana.
    Lakini Kamati ya Usajili ya Simba SC kwa pamoja na benchi la Ufundi wana mipango yao waliyojiewekea na wamekuwa wakisistizana kufanya usajili ndani ya mipango na taratibu walizojiwekea.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: BONGE LA BEKI LAOTA MBAWA SIMBA SC, MSIMBAZI SASA... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top