• HABARI MPYA

    Sunday, July 26, 2015

    YANGA SC WAMEPATA KATIBU WA AINA YAKE SAFARI HII!

    UBABE, uonevu, ukandamizaji ndiyo imekuwa desturi ya klabu kongwe nchini Simba na Yanga kwa muda mrefu.
    Kuchukua wachezaji wa timu ndogo kwa ubabe bila kufuata taratibu na hata wakati mwingine kuwa tayari kuhonga kwenye vyombo vya juu vyenye mamlaka kisoka ili mradi kutimiza dhuluma yao.
    Imeshuhudiwa miaka ya nyuma Simba na Yanga SC zikipora wachezaji wa timu nyingine bila kufuata taratibu, tu kwa sababu zenyewe ni timu kongwe zinazopendwa na watu wengi.

    Mwishoni mwa mwaka jana, Yanga SC ilipata mchezaji chipukizi kutoka timu ya Daraja la Kwanza, Kemondo ya Mbeya, aitwaye Godfrey Mwashiuya.
    Mchezaji huyo ni kama alijipeleka mwenyewe Yanga SC, hakutaka kusubiri bahati ya kutakiwa na timu kubwa, na labda iliyo ndani ya damu yake.
    Alijiunga na Yanga SC mapema bila kujali maslahi yake, dua yake kubwa ikiwa ni kuomba wakati ufike asajiliwe rasmi na kuwa mchezaji wa Yanga SC.
    Naam, wakati ukafika, mchezaji akapewa fomu za Mkataba na kusaini, kwa fedha kiasi gani ni siri yake na klabu yenyewe.
    Lakini baada ya kupewa nafasi na kucheza kwa mara ya kwanza Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo dhidi ya SC Villa mapema mwezi huu, Mwashiuya akaudhihirishia umma kwamba Yanga hawakukosea kumsajili.
    Alionyesha uwezo ambao mara moja ukageuka kuwa gumzo kubwa nchini- wengi wakimfananisha na mmoja wa mawinga bora kabisa kuwahi kutokea nchini, Edibily Jonas Lunyamila.
    Wakati wote Mwashiuya akiwa na Yanga SC tangu meishoni mwa mwaka jana, haikuwahi kutokea klabu inasema inatafuta mchezaji wake ametoweka.
    Na haikuwahi kutokea klabu kulalamika kwamba imesikia mchezaji wake yuko mazoezini na Yanga SC- kwa sababu kipindi chote hicho Mwashiuya amekuwa akifanya mazoezi na timu hiyo Dar es Salaam, akiwa amewekwa katika hoteli.
    Lakini baada ya kuonekana akiichezea Yanga SC kwa mara ya kwanza Uwanja wa Taifa, ndipo Kemondo wakaibuka na kuanza kulalamika kwamba mchezaji wao amechukuliwa kinyume na utaratibu.
    Mkuu waa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga SC, Jerry Muro akaibuka kuwajibu kupitia vyombo vya Habari akiwatolea maneno ya kejeli, kubwa walikuwa wapi muda wote huo.
    Yanga SC imekaa na Mwashiuya tangu mwaka jana, iweje leo baada ya kucheza ndipo iibuke timu inasema ni mchezaji wake? Hilo lilikuwa swali la Muro.
    Lakini huku Muro ‘akibwabwaja’ kwenye vyombo vya Habari, Katibu wa Yanga SC, Dk. Jonas Tiboroha akaenda kijijini kabisa Kemondo kwenda kuzungumza na uongozi wa klabu hiyo.
    Dk Tiboroha akagundua Kemondo ni klabu iliyomlea Mwashiuya kisoka na kweli ilikuwa ina Mkataba naye- hata kama uwe na mapungufu.  
    Dk Tiboroha akaona kabisa Yanga SC inapaswa kumalizana kistaarabu na klabu hiyo- na akafanya hivyo na Kemondo ikatoa baraka zote kwa Yanga SC kumchukua Mwashiuya.
    Kana kwamba hiyo haitoshi, Dk. Tiboroha akaenda hadi nyumbani kwao Mwashiuya, akajionea hali ya maisha ilivyo ngumu pale kijijini.
    Bila shaka alijuliza amempata kwa kiasi gani cha fedha Mwashiuya- na kulingana na uwezo wake kama angemkuta Mtibwa Sugar, Mbeya City au Coastal Union angempata kwa kiasi gani cha fedha.
    Kwa sababu hiyo, Tiboroha akawapa fedha familia ya Mwashiuya, ndipo akarejea Dar es Salaam.
    Faida za alichokifanya Dk. Tiboroha sasa Kemondo ni marafiki wa Yanga SC na watu wengi wa Mbeya watakayoipata historia hiyo, wataipenda Yanga SC.
    Familia ya Mwashiuya imefarijika na imetoa Baraka zake zote kwa kijana wao akacheze mpira Yanga SC. Mchezaji mwenyewe sasa ana amani ya kutosha kufanya kazi Yanga SC. Ni dalili nzuri kwamba atafanikiwa.
    Baada ya kumaliza sakata la Mwashiuya, likajitokeza sakata la mchezaji mwingine, kipa Mudathir Khamis wa KMKM ya Zanzibar.
    Wakati Yanga SC inamsajili kipa huyo, Mudathir alisema hana Mkataba- lakini bahati mbaya KMKM wakaibuka na kusema wana Mkataba naye.
    Kwa mara nyingine, Dk. Tiboroha hakutaka malumbano ya kwenye vyombo vya habari, akapanda boti hadi Zanzibar kwenda kuzungumza na uongozi wa KMKM.
    Yanga SC na KMKM wamalizana vizuri na hatimaye Mudathir ameridhiwa kuhamia Dar es Salaam kikazi.
    Na katika usajili mzima wa Yanga SC, hakuna malalamiko yoyote tangu Tiboroha ameingia kazini, yawe mchezaji au timu dhidi ya Yanga SC.
    Huyu ni aina mpya kabisa ya Katibu kati ya Makatibu waliowahi kutokea Yanga SC. Ni aina ya viongozi ambao soka ya Tanzania inawahitaji.
    Historia yake inaonyesha aliingia Yanga SC kutokea TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) na ni msomi kweli, ilikuwaje Jamal Malinzi (Rais wa TFF) akamuachia aondoke? Sijui.
    Mwaka huu Yanga SC wamepata Katibu Mkuu wa aina yake. Alamsiki. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC WAMEPATA KATIBU WA AINA YAKE SAFARI HII! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top