• HABARI MPYA

    Friday, July 31, 2015

    MAGURI AFIKISHA MABAO 10 SIMBA SC BAADA YA MECHI 40

    Elias Maguri amefunga bao lake la 10 Simba SC jana katika mechi yae 40 tangu atue Msimbazi
    MSHAMBULIAJI wa Simba SC, Elias Maguri jana amefunga bao lake 10 tangu ajiunge na Simba SC Juni mwaka juzi kutoka Ruvu Shooting ya Pwani.
    Maguri amefunga bao la 10 tangu atue Simba akiichezea kwa mara ya 40 klabu hiyo ikishinda 4-0 katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Black Sailor Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Maguri alikuwa ana mwanzo mzuri Simba SC chini ya kocha Patrick Phiri akifunga bao dhidi ya mahasimu, Yanga katika mechi yake ya Nani Mtani Jembe, lakini mambo yalianza kumuendea kombo taratibu baada ya Mzambia huyo kuondoka.
    Maguri akawa mchezaji wa kutokea benchi mara nyingi chini ya kocha Mserbia, Goran Kaponovic aliyeondoka mwishoni mwa msimu baada ya kutofikia makubaliano na uongozi juu ya Mkataba mpya.
    Lakini sasa, chini ya kocha mpya Muingereza, Dylan Kerr dalili za nyota ya Maguri, mshambuliaji mwenye nguvu, kasi na uwezo wa kuutunza mpira kung’ara tena zimeanza baada ya jana kufungwa.
    Simba SC imeweka kambi Zanzibar kujiandaa na msimu mpya na Agosti 8 inatarajiwa kucheza na AFC Leopard ya Kenya katika tamasha la Simba Dar.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAGURI AFIKISHA MABAO 10 SIMBA SC BAADA YA MECHI 40 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top