Kiungo mshambuliaji chipukizi wa Yanga, Simon
Msuva anatakiwa kubadilika kwa kuachana na kucheza soka ya kibinafsi na badala
yake kucheza kwa maslahi ya timu, Msuva amekuwa akicheza kama yupo peke yake
uwanjani, hawaangalii wenzake wapo katika nafasi gani ili aweze kuwapatia
mipira. Anaweza akapewa mpira kwenye njia akachomoka nao vizuri, lakini
akikaribia kwenye eneo la hatari, atataka kulazimisha kufunga mwenyewe hata
kama hayuko kwenye nafasi nzuri, dhahiri desturi hiyo, imemfanya kocha wa timu
ya taifa, Mdenmark Kim Poulsen sasa aanze kmumsahau benchi. Kim alianza kumpiga
benchi winga huyo katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati,
CECAFA Tusker Challenge nchini Uganda mwezi huu, lakini bado inaonekana kijana
huyo hajapata fundisho lolote, kwani ameendelea na desturi hiyo. Katika mchezo
wa kirafiki wa timu yake, Yanga dhidi ya Tusker jana Msuva alichangia
kuikosesha timu yake ushindi kwa uchoyo wake. Alishindwa kumpa pasi mara mbili
Jerry Tegete akiwa kwenye nafasi nzuri. Hii imanaanisha, Kocha wa Yanga,
Mholanzi Ernie Brandts atakapochoshwa na desturi yake hiyo, anaweza kuamua
kuanza kumuweka benchi na huo ukawa mwanzo wake wa kupotea kwenye ramani ya
soka baada ya muda mfupi tangu aibuke. Ipo haja ya Msuva (pichani) kubadilika. Ni
mchezaji mzuri, ana kasi, uwezo wa kumiliki mpira na kipaji, lakini ubinafsi unahatarisha
nafasi yake uwanjani. |