• HABARI MPYA

    Thursday, December 27, 2012

    MTU WA WATU, RIDHIWANI KIKWETE MGENI RASMI MKUTANO MKUU TASWA

    Ridhiwani, mtu wa watu

    Na Amir Mhando
    MAANDALIZI ya Mkutano Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) yanaenda vizuri na wajumbe wanatarajiwa kufika Bagamoyo kesho (Desemba 28, 2012) mchana kwenye hoteli ya Kiromo View Resort watakapolala na kufanyia mkutano.
    Ijumaa hiyo washiriki watatembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria Bagamoyo na jioni kutakuwa na mechi ya kirafiki kati ya timu ya soka ya TASWA FC na Bagamoyo Veterani itakayofanyika Uwanja wa Mwanakalenge na usiku wajumbe watakuwa na chakula cha pamoja na kubadilishana mawazo kuhusiana na masuala mbalimbali yahusiyo michezo na taaluma ya habari.
    Mkutano Mkuu utafunguliwa Jumamosi Desemba 29, saa tatu asubuhi na mgeni rasmi atakuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kusaidia timu za Taifa za Vijana, Ridhiwani Kikwete.TASWA imechukua jukumu la kumualika kutokana na kuwa mdau mkubwa na rafiki wa chama chetu.
    Mkutano utafungwa jioni ya siku hiyo na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene ambaye hiyo pia itakuwa nafasi nzuri kwake kuweza kuzungumza na wana habari kuhusiana na masuala mbalimbali ya kitaaluma.
    Katika mkutano huo wanachama wa TASWA watapata fursa ya kupokea na kujadili Ripoti ya Utendaji ya chama, Mapato na Matumizi, maendeleo ya chama na masuala mbalimbali yanayohusu waandishi wa habari za michezo na maendeleo ya michezo kwa ujumla
    Pia kutakuwa na semina maalum itakayoendeshwa kwa washiriki wa mkutano huo, ili wawe na uelewa kuhusiana na ajenda ya kuinua kipato kwa wanachama ambayo nayo itajadiliwa kwenye mkutano huo.
    Kamati ya Utendaji ya TASWA imekubaliana iwasaidie wanachama wake waweze kujitegemea kwa kuanzisha Chama cha Akiba na Mikopo (SACCO’S), lakini imeamua kwanza iwaite wataalamu wa vyama vya ushirika watoe elimu juu ya jambo hilo na kukishakuwa na uelewa wa kutosha suala hilo litakuwa kama ajenda kamili ya kuanzisha chama hicho kwenye mkutano wetu.
    (Mwandishi wa habari hizi ni Katibu Mkuu wa TASWA)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: MTU WA WATU, RIDHIWANI KIKWETE MGENI RASMI MKUTANO MKUU TASWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top