Hakuwa mchezaji wa kikosi cha kwanza cha Yanga
katika mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na mara nyingine
amekuwa akimalizia benchi dakika zote za mchezo, kuanzia Klabu Bingwa Afrika
Mashariki na Kati, Kombe la Kagame. Lakini mara zote chache alipoinuliwa
kutokea benchi, kiungo Nizar Khalfan amekuwa akionyesha yeye ni mtu anayepaswa
kuwa uwanjani muda wote. Hata jana Nizar, alitokea benchi katika mchezo wa
kirafiki dhidi ya Tusker ya Kenya, akacheza soka maridadi, akiwatengenezea
wenzake nafasi na hata kujaribu mwenyewe kufunga. Alikuwa anakaba kila timu ilipopoteza
mipira na kwa ujumla alikuwa anacheza kwa manufaa ya timu. Huyu ni mchezaji
mwenye uzoefu aliyecheza soka ya kulipwa Asia na Amerika. Amecheza Ligi kubwa
pamoja na wachezaji kama Thierry Henry na David Beckham nchini Marekani. Amecheza
mechi nyingi za kimataifa na amefanya mambo makubwa ya kihistoria, ikiwemo
kumtungua bao tamu sana kipa wa Senegal, Tony Silva. Huwezi kuona sababu ya
Nizar kuwekwa benchi Yanga. |