• HABARI MPYA

    Sunday, December 23, 2012

    TUNAJIDANGANYA NA KWA MTAJI HUU HATUTAFIKA POPOTE

    Na Mahmoud Bin Zubeiry

    MICHUANO ya vijana chini ya umri wa miaka 20 ya klabu za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, maarufu kama Kombe la Uhai, inatarajiwa kufikia tamati leo kwa mchezo wa fainali kati ya Coastal Union ya Tanga na Azam kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
    Timu hizo zimepata fursa hiyo baada ya kushinda mechi zao za nusu fainali ya michuano hiyo inayoshirikisha timu za vijana wenye umri chini ya miaka 20 za klabu za Ligi Kuu ya Vodacom jana. Michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia maji Uhai.
    Azam ndiyo iliyokuwa ya kwanza kupata tiketi ya fainali baada ya kuitoa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwa mikwaju ya penalti 3-2, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 90, wakati Coastal Union iliivua ubingwa Simba kwa kuifunga mabao 2-1.
    Mechi ya fainali itaanza saa 10 kamili jioni, na itatanguliwa na ile ya kutafuta mshindi wa tatu kati ya Mtibwa Sugar na Simba ambayo itachezwa saa 2 kamili asubuhi kwenye uwanja huo huo.
    Mbali ya kombe, bingwa wa michuano hiyo atapata sh. milioni 1.5, makamu bingwa sh. milioni 1 wakati mshindi wa tatu atajinyakulia sh. 500,000. Timu iliyoonesha zaidi mchezo wa kiungwana (fair play) itapata sh. 400,000, mchezaji bora wa mashindano sh. 350,000, mfungaji bora sh. 300,000 na kipa bora sh. 300,000.
    Naye kocha bora katika mashindano hayo atazawadiwa sh. 300,000 kama itakavyokuwa kwa refa bora.
    Rais wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Sepp Blatter alikwishasema lengo ya wao kutilia mkazo na kuimarisha mashindano ya vijana ni kuandaa nyota wa baadaye wa soka.
    Na unaweza kuona nyota wengi wanaowika katika soka duniani hivi sasa, wametokea katika mashindano hayo ya vijana.
    John Michael Nchekwube Obinna ama Mikel John Obi au John Obi Mikel wa Nigeria aliibukia kwenye michuano ya U17 ya dunia mwaka 2003 iliyofanyika katika miji ya Helsinki, Tampere, Lahti na Turku nchini Finland.
    Japokuwa Nigeria haikufua dafu kwenye Kundi lake B, lililokuwa na timu za Argentina iliyoongoza kwa pointi zake tisa, Costa Rica iliyofuatia kwa pointi zake nne sawa na Nigeria na kuzidiwa kwa wastani wa mabao tu, lakini soka nzuri ya Obi ilimuuza na sasa mchezaji mkubwa Ulaya.
    Hajatwaa tuzo ya Mwanasoka Bora wa Afrika, ndiyo- lakini ana Medali ya dhahabu ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na anachezea klabu kubwa, analipwa vizuri. Ni tajiri kutokana na soka.
    Lionel Andres Messi au ‘Leo Messi’ aling’ara katika Kombe la Dunia la U20 mwaka 2005 nchini Uholanzi, akiiwezesha Argentina kuwa bingwa naye akishinda tuzo za Mchezaji Bora wa mashindano na mfungaji bora wa fainali hizo pia.
    Leo huyu bila kujiumauma dunia inakiri ndiye mchezaji bora zaidi mwenye kipaji cha kipekee, ambaye akiwa ametia kibindoni tuzo tatu za Mwanasoka Bora wa Dunia, bado jibu linakuwa gumu kama si yeye tuzo ya mwaka huu apewe nani mwingine?
    Kwa ujumla michuano ya vijana ni muhimu mno kumuandaa mchezaji bora wa baadaye, wataalamu wanasema ki professional, hatua kwa hatua U17, U20, U23 na baada ya hapo anakuwa mchezaji kamili, mwenye kustahili kuitwa senior.
    Lakini ajabu imetokea desturi mbaya sana katika mashindano ya vijana hapa Tanzania, timu zinaingiza wachezaji waliozidi umri katika mashindano.
    Desturi hii wanayo sana watu wa Afrika Magharibi na imekwishawaumbua sana kwa wachezaji kugundulika wamedanganya umri na hilo limepunguza soko la wachezaji wa Nigeria duniani.
    Tukienda kwenye dhana halisi ya mashindano ya vijana, ambayo ni kumuandaa mchezaji wa kesho, dhahiri ni kupoteza muda na kujidanganya wenyewe kwa kutumia wachezaji waliozidi umri kwenye mashindano.
    Tazama Kombe la Uhai mwaka huu, imeshuhudiwa wachezaji wanarudi kwa mara ya nne katika vikosi vyao, eti bado U20 na ukitazama hata mwonekano wao, dhahiri unapata picha ya udanganyifu.
    Bodi za soka haziwezi kusimamia kila kitu au kuwa na wepesi wa kugundua kila kitu cha uongo, ikiwa wanaodanganya wanakuwa wamejipanga kuhalalisha uongo wao.
    Lakini pamoja na yote, kuna kiwango ambacho anafikia mchezaji na baada ya hapo hupaswi kumrudisha chini, bali anatakiwa kuendelea kukomazwa na kujengwa zaidi huko juu, ili kutoa nafasi ya kuandaa vijana wengine.
    Ramadhani Singano, Edward Christopher wote ni hawa ni wachezaji wa kikosi cha kwanza cha Simba na timu ya taifa, Taifa Stars- kuwarudisha chini ni kuwarudisha nyuma wao wenyewe, bila hata kuangalia umri wao.
    Au Simon Msuva na Frank Domayo, wote hawa ni wachezaji wa kikosi cha kwanza cha Yanga na timu ya taifa, hawapaswi kurudishwa chini na ndiyo maana Samuel Eto’o tangu aweke rekodi ya kuwa mchezaji mdogo zaidi kucheza Fainali za Kombe la Dunia Juni 17, mwaka 1998, hakuwahi kurudishwa chini, zaidi tu ya kuchezea kikosi cha Olimpiki mwaka 2000 kilichoshinda Medali ya Dhahabu.
    Akiwa na umri wa miaka 17 na miezi mitatu, Eto’o aliichezea Cameroon nchini Ufaransa ikilambwa 3–0 na Italia katika hatua ya makundi na baada ya hapo akawa mchezaji wa kudumu wa kikosi cha wakubwa cha Simba Wasiofungika.
    Sababu ya FIFA kuamua kuleta vipimo vya kubaini umri halisi wa wachezaji ni kutokana na kuona dhana yao ya mashindano ya vijana inapotoshwa- watu wamekuwa wagumu kuelewa na ndiyo maana ukifuatilia wachezaji wa Afrika miaka ya karibuni wanaibuka na kupotea baada ya mfupi.
    Siku moja Tanzania tukiamua kufuata misingi halisi ya soka na miiko yake, tutafanikiwa, lakini kama tutaendelea na usanii wetu, basi tutaendelea kuwa watu wa kubahatisha bahatisha tu na hatutafika popote.
    Sasa tuamue kutumia vema mashindano ya vijana kwa kutumia wachezaji wanaostahili au kuendelea kuweka vijeba kwa tamaa ya kutwaa ubingwa, lakini mwisho wa siku hatujengi?
    Tunajidanganya, tunawapotezea muda wachezaji na mwisho wa siku watadumaa bila kufika popote. Ndiyo, kuwafanya wao watoto siku zote ni kuwadumaza hata kiakili. Wasalam! 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: TUNAJIDANGANYA NA KWA MTAJI HUU HATUTAFIKA POPOTE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top