• HABARI MPYA

    Tuesday, October 02, 2012

    KUELEKEA PAMBANO LA WATANI, MINZIRO KESHO...

    Minziro kulia akiwa na Samatta

    Na Mahmoud Zubeiry
    FREDDY Felix Isaya Kataraiya ‘Minziro’ au Majeshi kwa jina lingine la utani, kesho ataiongoza Yanga kwa mara ya pili mfululizo kama kocha Mkuu kwenye mechi dhidi ya watani wa jadi, Simba SC, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Minziro amekuwa kocha Yanga kwa muda mrefu na kwa vipindi tofauti, tangu mwaka 1997, lakini kwa kipindi chote hicho amekuwa Kocha Msaidizi, ila dharula zilizojitokeza siku za karibuni zimekuwa zikimuangushia kwenye kuaminiwa kuongoza timu katika mechi nzito.
    Kama ilivyokuwa katika mechi iliyopita, Mei 6, mwaka huu, Minziro aliachiwa timu wastani wa wiki mbili kabla ya mechi na watani na safari hii inakuwa hivyo, ameachiwa timu ndani ya wastani wa muda huo.
    Msimu uliopita, Minziro aliachiwa timu baada ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Mserbia Kostadin Bozidar Papic kutimuliwa, na safari hii anaachiwa timu baada ya Mbelgiji, Tom Saintfiet pia kutimuliwa.
    Ingawa Yanga imekwishaleta kocha mpya, Ernie Brandts kutoka Uholanzi lakini rasmi bado hajaanza kazi kutokana na kutokamilishiwa kwa baadhi ya taratibu za kikanuni- hivyo sana atakuwa na wasaa wa kutoa ushauri tu nje ya Uwanja.
    Jahazi kesho litaongozwa na Minziro, ambaye atakuwa akisaidiwa na kocha wa makipa, Mfaume Athumani Samatta, wale wale waliopigwa 5-0 na Simba SC. Mechi za Simba na Yanga zina ugumu wake kwa sababu zina mambo mengi sana.
    Ingekuwa kazi rahisi kwa Minziro kukutana na Simba akiwa kocha wa timu yoyote, lakini si Yanga na dhahiri usiku wa kuamkia kesho kwake utakuwa mzito sana, akiitafakari mechi hiyo, na hasa akikumbuka zile 5-0 za Mei 6.
    Mechi ya kesho itakuwa na sura mbili kwa Minziro, kumjenga au kumbomoa mbele ya wana Yanga. Timu ikifanya vizuri itamjenga, lakini ikirudia madudu ya Mei 6- hakika atakuwa kwenye wakati mgumu mno.
    Dhahiri Yanga watamtazama mara mbili Minziro, kama kweli wanaye kocha sahihi Msaidizi, ambaye anaweza kukaimu majukumu ya bosi wake wakati wowote ikitokea dharula, au wana mtu tu kwenye benchi?
    Kama itakumbukwa, staili kama hizi za kocha mkuu kupata dharula ndizo zilimuinua Jamhuri Mussa Kihwelo ‘Julio’ pale Simba- kwani aliachiwa timu na akawafunga Yanga Morogoro hata sasa naye amekuwa ‘Super Coach’.
    Vivyo hivyo kwa Minziro, kesho itakuwa siku ya mtihani mzito kwake, ambao vema kwake afaulu, lakini akifeli sijui awe na bahati gani tu hata aendelee kuwa kocha wa Yanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KUELEKEA PAMBANO LA WATANI, MINZIRO KESHO... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top