• HABARI MPYA

    Tuesday, September 19, 2017

    OKWI: TANZANIA KUNA WACHEZAJI WENGI WAZURI, LAKINI MIMI NINAVUTIWA NA KAMUSOKO NA NGOMA

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Arnold Okwi amesema kwamba anavutiwa na wachezaji wawili wa kigeni katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, ambao ni Wazimbabwe kiungo Thabani Kamusoko na mshambuliaji Donald Ngoma.
    Mshambuliaji huyo wa Simba, Okwi amewasifu wachezaji hao wa timu yake ya zamani, Yanga jana mjini Dar es Salaam katika hafla fupi ya kukabidhiwa tuzo yake ya Mchezaji Bora wa Mwezi Agosti wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    “Kwa Tanzania klabu nyingi zina wachezaji wazuri, lakini nje ya Simba kuna mchezaji anaitwa Kamusoko ananivutia sana na Donald Ngoma pia,” alisema Okwi jana baada ya kukabidhiwa tuzo yake, pamoja na donge nono la Sh. Milioni 1 kwa ushindi wake huo.
    Okwi alikabidhiwa zawadi hizo na Meneja Chapa wa Vodacom Tanzania, Yvonne Maruma aliyeambatana na Afisa Udhamini, Ibrahim Kaude ambao pia walimpongeza Mganda huyo kwa kuwa na mwanzo mzuri akirejea Ligi Kuu kwa mara ya pili. 
    Okwi ameshinda tuzo hiyo baada ya mechi moja tu, akifunga mabao manne dhidi ya Ruvu Shooting Agosti 26, Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, Simba SC ikipata ushindi wa 7-0 kwenye mechi hiyo ya ufunguzi.
    Na haitakuwa ajabu kwa Okwi kushinda na tuzo ya Septemba pia, baada ya kuendeleza moto wake wa mabao, kufuatia kufunga mabao mawili katika ushindi wa 3-0 dhidi ya Mwadui FC mwishoni mwa wiki.
    Donald Ngoma akimpita beki Mzimbabwe mwenzake wa Simba, Method Mwanjali  
    Thabani Kamusoko (kulia) akipiga mpira dhidi ya kiungo Mnyarwanda wa Simba, Haruna Niyonzima

    Okwi yupo Simba SC kwa mara ya tatu, baada ya awali kucheza na kuondoka mara mbili. Aliwasili Msimbazi kwa mara ya kwanza mwaka 2010 akitokea SC Villa ya kwao, Uganda na akacheza hadi mwaka 2013 alipohamia Etoile du Sahel ya Tunisia, ambako hakudumu akarejea Uganda kujiunga na SC Villa mwaka huo huo, ambako pia alikaa kwa miezi michache kabla ya kuja Tanzania kujiunga na mahasimu, Yanga.
    Alicheza Yanga kwa nusu msimu hadi mwaka 2014 aliporejea Simba ambako alicheza hadi mwaka 2015 alipohamia Sonderjyske ya Denmark alikodumu hadi mapema mwaka huu aliporejea tena SC Villa, kabla ya Julai kusaini tena Simba ambako yuko kwa mara ya tatu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OKWI: TANZANIA KUNA WACHEZAJI WENGI WAZURI, LAKINI MIMI NINAVUTIWA NA KAMUSOKO NA NGOMA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top