• HABARI MPYA

    Thursday, May 23, 2013

    HOYCE TEMU KUWATEMBELEA MISS KIGAMBONI KESHO

    Washiriki wa Miss Kigamboni wakiwa mazoezini leo Break Pointi, katikati ya Jiji la Dar es Salaam
    Na Princess Asia, IMEWEKWA MEI 23, 2013 SAA 12:55 JIONI 
    MREMBO wa Tanzania mwaka 1999, Hoyce Temu, leo anatarajia kukutana na washiriki wanaowania taji la kitongoji la Kigamboni mwaka huu "Redd's Miss Kigamboni 2013" ili kuwapa nasaha mbalimbali kuhusiana na sanaa hiyo. Shindano la Redd's Miss Kigamboni linatarajiwa kufanyika Ijumaa Juni 7 kwenye ukumbi wa Navy Beach kuanzia saa 2:00 usiku hapa jijini Dar es Salaam. Akizungumza na gazeti hili jana, Mratibu wa shindano hilo, Somoe Ng'itu, alisema kuwa maandalizi ya shindano hilo yako katika hatua za mwisho na lengo la kumualika Hoyce ni kutaka kuwapa nafasi warembo kujifunza mambo mbalimbali yanayohusu sanaa hiyo. Mratibu huyo alisema kuwa washiriki hao watajifunza mambo ya msingi kupitia mrembo huyo ambaye pia atawapa uelewa wa mbinu watakazokutana nazo kwenye mashindano ya Kanda, taifa na baadaye fainali za dunia. "Ni fursa ambayo tunatarajia warembo wetu wapate, nia ya kufanya hivi ni kuwaandaa kufanya vizuri, tumejipanga kupata mafanikio zaidi ya tuliyovuna mwaka jana," alisema Somoe. Aliongeza kuwa mpaka sasa jumla ya warembo 12 wanaendelea na mazoezi hapa jijini chini ya Blessing Ngowi. Aliwataja washiriki hao kuwa ni pamoja na Rogathe Michael, Irene Rajab, Magdalena Olotu, Latifa Mohammed, Axsaritha Vedastus, Angella Lutataza, Sara Makembo, Amina Mussa, Ellen Sulle, Julieth Mwanri na Rachel Reuben. Aliyataka makampuni na taasisi mbalimbali zinakaribishwa kudhamini shindano hilo ambalo mwaka jana lilitoa mshindi katika kinyang'anyiro cha Kanda ya Temeke ambaye ni Edda Sylivester. Warembo watano watakaoshika nafasi za juu kwenye shindano hilo watapata nafasi ya kushiriki kinyang'anyiro cha Redd's Miss Temeke baadaye mwaka huu. Wadhamini ambao wamethibitisha kusaidia shindano hilo ni pamoja na kampuni ya bia Tanzania kupitia kinywaji cha Redd's Premium Original, Montage Limited, Clouds Media Group, Papa Z na Break Point. Taji la Redd's Miss Tanzania linashikiliwa na Brigitte Alfred wakati Edda alishika alifanikiwa kushika nafasi ya tatu kwenye fainali hizo za taifa mwaka jana.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: HOYCE TEMU KUWATEMBELEA MISS KIGAMBONI KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top