• HABARI MPYA

    Thursday, February 21, 2013

    TBL YAWATAKA TFF WATUMIE BASI LA STARS KWA MANUFAA YA TIMU

    Basi la Stars

    Na Prince Akbar
    KAMPUNI ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia yake ya Kilimanjaro, leo hii imekabidhi basi jipya kwa Timu ya Taifa (Taifa Stars), likiwa na thamani ya zaidi ya Sh milioni 200 kwa udhamini wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager.
    Hafla ya makabidhiano imefanyika Makao Makuu ya TBL jijini Dar es Salaam na kupewa Baraka na Mkurugenzi Mkuu wa TBL, Robin Goetzsche. Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na maofisa kutoka TFF, wafanyakazi za TBL, wadau wa soka na vyombo mbalimbali vya habari.
    TBL imenunua basi hilo ikiwa ni sehemu ya ufadhili kama ilivyoanishwa katika mkataba baina ya pande hizo mbili. Mkataba huo ulitiwa saini Mei mwaka jana na lengo kuu ni kuinua kiwango cha Taifa Stars.
    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TBL alisema: Imeshatimia miezi 10 tangu tuanze kuifadhili  Taifa Stars na malengo yetu kama wadhamini ni kuiona timu ikipata ushindi uwanjani ma hivyo kuongeza sifa ya timu na tumeridhika na matokeo.”
    Mkurugenzi huyo alisema, kukabidhi kwa basi hilo ni ishara kwamba TBL itaendelea kuisadia timu ya taifa na hivyo kupandisha kiwango cha soka nchini na aliwataka wahusika kulitunza basi hilo kwa manufaa ya timu na taifa kwa ujumla. “Tutaendelea kutoa msaada na tunatarajia kuwa nanyi kwa nafasi yenu mtafanya bidii na hivyo kutupa moyo wa kuendelea na uwekezaji. Tunaamini mtafanya vizuri katika mechi nyingi za kimataifa na hivyo kupanda kwenye viwango vya FIFA.”
    Kwa upande wake, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, George Kavishe alisema basi hilo lenye uwezo wa kubeba abiria 51, limenunuliwa kutoka Yutong na thamani yake  ni zaidi ya Sh milioni 200.
    Akitoa ufafanuzi, Kavishe alisema basi hilo kutoka Kampuni ya Yutong lina Chassis ya 4X2, uwezo wa injini ni 300 HP Cummins, huku likiwa na uwezo wa kumeza lita 800 za mafuta. Mbali na hayo kila siti ina mkanda wa abiria kwa ajili ya usalama wakati wa safari, luninga mbili, redio yenye spika nane, mafriji mawili, viyoyozi na milango ya kisasa inayojifungua na pia nafasi kutoka kiti kimoja hadi kingine ni kubwa.
    “Wachezaji wetu lazima wawe na nafasi nzuri ya kupumzika wakati wa safari, na hiyo ndiyo sababu iliyotufanya tumumue basi hili la kisasa zaidi likiwa na vifaa muhimu ambavyo pia ni vya kisasa…tunawaomba kulitunza basi hili,” alisema Kavishe na kuongeza kuwa ni jukumu lao kufanya hayo kwa mujibu wa mkataba ili kuinua kiwango cha timu.
    Baada ya makabidhiano hayo, basi lilifanya ziara katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam ili mashabiki walione na kupiga picha huku kukiwa na matukio kadhaa ya kusisimua kama vile kucheza na kuimba.
    Naye Rais wa TFF, Leodgar Tenga aliipongeza TBL kwa udhamini wake wa uhakika na kusisitiz akuwa tangu wameanza wameshatekeleza ahadi walizoahidi na moja wapo ikiwa ni kuhakikisha basi jipya linanunuliwa.
    “Hawajawahi kuchelewesha malipo hata mara moja na kwa hilo tunawashukuru sana,” alisema Rais Tenga.
    Bia ya Kilimanjaro ilianza kuifadhili Taifa Stars Mei mwaka jana kwa mkataba uliogharimu zaidi ya Sh bilioni 2 kwa mwaka katika kipindi cha miaka mitano na TFF.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: TBL YAWATAKA TFF WATUMIE BASI LA STARS KWA MANUFAA YA TIMU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top