• HABARI MPYA

    Saturday, February 23, 2013

    NIYONZIMA AIPAISHA YANGA, REFA AOKOLEWA NA POLISI

    Haruna Niyonzima akipoza koo kwa maji baada ya kuifungia Yanga bao leo
    Na Mahmoud Zubeiry
    YANGA SC imejitanua kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kufuatia ushindi wa bao 1-0 jioni hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam dhidi ya Azam FC. 
    Matokeo hayo, yanaifanya Yanga itimize pointi 39, baada ya kucheza mechi 17, hivyo kuendelea kuongoza Ligi Kuu, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 36 ambayo pia imecheza mechi moja zaidi. 
    Hadi mapumziko, Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0, lililofungwa kitaalamu na kiungo Haruna Niyonzima aliyepokea pasi ya Jerry Tegete.
    Lilikuwa bao tamu, lililotokana na mpangilio mzuri wa shambulizi, Yanga wakigongeana pasi kutokea nyuma hadi kwenye eneo la hatari la Azam.
    Refa Hashim Abdallah akitolewa kwa ulinzi wa Polisi leo
    Mshambuliaji Jerry Tegete leo bahati haikuwa yake, kwani aliikosesha Yanga mabao ya wazi katika dakika za 40, 44 na 61, akiwa kwenye nafasi nzuri za kufunga.  
    Azam nao walipoteza nafasi tatu nzuri za kufunga, mbili kupitia kwa Kipre Tchetche dakika ya 59 na 61 na nyingine John Bocco ‘Adebayor’ dakika ya 67.  
    Katika mchezo huo, kipindi cha kwanza Yanga walitawala zaidi na kufanya mashambulizi mengi ya hatari, lakini kipindi cha pili Azam ndio waliotalawa zaidi na kukaribia kusawazisha.
    Katika kupunguza kasi ya Azam, kipa wa Yanga, Ally Mustafa ‘Barthez’ alikuwa akijiangusha angusha mara kwa mara ili kupoteza muda, kiasi cha kupewa kadi ya njano na refa Hashim Abdallah. 
    Wachezaji wa Azam wakiongozwa na John Bocco ‘Adebayor’ walimvamia refa Hashim baada ya mchezo, wakimlalamikia kumaliza mchezo kabla ya muda. 
    Kutokana na tafrani hiyo, ilibidi Polisi waingie uwanjani kuwatoa marefa chini ya ulinzi wao na walipofika kwenye mlango wa kuingilia vyumbani mwao, mashabiki wa Simba walianza kuwatupia chupa.
    Kocha wa Azam, Muingereza Stewart Hall alianza kwa kuwapongeza Yanga na akasikitika hawakucheza vema kuweza kushinda, hususan kipindi cha kwanza, lakini kipindi cha pili walijaribu, ingawa alisema wapinzani wake walikuwa bora katika ulinzi.
    Kocha wa Yanga, Mholanzi Ernie Brandts alisema vijana wake walicheza vema kipindi cha kwanza, lakini kipindi cha pili walipoteza mwelekeo na akashukuru mno bao la Niyonzima limempa pointi tatu. 
    Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Simon Msuva, Frank Domayo, Jerry Tegete/Didier Kavumbangu, Hamisi Kiiza/Said Bahanuzi na Haruna Niyonzima.
    Azam FC; Mwadini Ally, Kipre Balou/Jabir Aziz, Waziri Salum, Joackins Atudo, David Mwantika, Ibrahim Mwaipopo, Salum Abubakar, John Bocco, Kipre Tchetche, Humphrey Mieno na Khamis Mcha ‘Vialli’/Seif Abdallah. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: NIYONZIMA AIPAISHA YANGA, REFA AOKOLEWA NA POLISI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top