• HABARI MPYA

    Tuesday, February 19, 2013

    SIMBA YATUA MBEYA KUIVAA PRISONS BILA KAPOMBE, MUDDE, MKUDE

    Kapombe akilia baada ya kuumia Jumapili. hajaenda Mbeya

    Na Mahmoud Zubeiry
    SIMBA SC ipo tayari mjini Mbeya kwa ajili ya mchezo wao wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, dhidi ya wenyeji Tanzania Prisons, utakaopigwa kwenye Uwanja wa Sokoine mjini humo.
    Huo utakuwa mchezo wa tatu kwa Simba SC tangu kuanza kwa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu, ikiwa imeshinda mechi moja tu 3-1 dhidi ya African Lyon na kutoa sare mbili, dhidi ya JKT Ruvu na JKT Oljoro, zote 1-1.
    Simba imefika Mbeya bila wachezaji wake nyota watano, ambao ni majeruhi, Jonas Mkude, Shomary Kapombe, Paul Ngalema, Christopher Edward na Mussa Mudde. Edward na Mkude wanasumbuliwa na maumivu ya nyama za paja, Mudde ameenda kwao Uganda kushiriki msiba wa mwanawe na Ngalema anasumbuliwa na maumivu ya goti.
    Kapombe aliumia misuli baada ya mechi dhidi ya Recreativo de Libolo ya Angola Jumapili na jana alifanyiwa vipimo katika hospitali ya Aga Khan, Dar es Salaam.
    Ofisa Habari wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga amesema kwamba majibu ya vipimo yanaonyesha Kapombe hana tatizo kubwa, bali misuli ilishituka kidogo.  
    Kamwaga amesema Kapombe ametakiwa kupumzika kwa siku nne, akipatiwa tiba za miale na atakuwa tayari kucheza mechi ijayo dhidi ya Mtibwa Sugar. 

    Kwa upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9 mwaka huu.
    Hekaheka nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha timu 14.
    Mwamuzi Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa timu zote mbili.
    Nayo JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15.
    Iwapo itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina pointi 33.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: SIMBA YATUA MBEYA KUIVAA PRISONS BILA KAPOMBE, MUDDE, MKUDE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top