• HABARI MPYA

    Thursday, March 29, 2012

    MATAJIRI YANGA WAMWAGA MAMILIONI MAZOEZINI COASTAL AFE JUMAMOSI


    Kikosi cha Yanga

    KAMATI ya Mashindano ya klabu ya Yanga, leo imewapa wachezaji wa klabu hiyo Sh. Milioni 5 wagawane na kuwaahidi Sh. Milioni 5 nyingine wakishinda mechi dhidi ya Coastal Union ya Tanga Jumamosi Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.Mchezo huo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzaania Bara unatarajiwa kuwa mkali na wa kusisimua, kwani Coastal inayofundishwa na wachezaji wawili wa kimataifa wa zamani nchini, beki Jamhuri Mussa Kihwelo na Juma Ramadhan Mgunda imepania kushinda kuitibulia Yanga harakati za ubingwa.
    Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu ameaimbia bongostaz muda mchache uliopita kwamba morali kuelekea mchezo huo ni kubwa mno na Yanga wamejipanga sawasawa kuhakikisha wanavuna pointi tatu.Sendeu alisema kwamba Yanga imefanya mazoezi Uwanja wa Kaunda leo na jana ilifanya Uwanja wa Tiper, Kigamboni wakati juzi ilifanya Uwanja wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Kijitonyama, Dar es Salaam.Alipoulizwa sababu za kubadilisha viwanja mara kwa mara, Sendeu alisema kwamba kocha wao, Mserbia Kostadin Bozidar Papic amekuwa akilalamikia ubovu katika viwanja vingi wanavyokwenda.Sendeu alisema kwamba Papic anaridhishwa zaidi na Uwanja wa shule ya sekondari Loyola, Mabibo, Dar es Salaam, ambao kwa sasa umefungwa kwa ajili ya ukarabati.“Anapapenda pale kwa sababu pia watu hawaangalii mazoezi, kuna uzio. Kwa hiyo anakuwa huru zaidi na kazi zake,”alisema.Kuhusu hali ya wachezaji, alisema ni Salum Abdul Telela pekee ambaye hatajumuishwa kwenye mchezo huo kwa sababu amepewa mapumziko baada ya kupona.“Huo ndio utaratibu wetu kwa sasa, mchezaji akipona anapewa muda zaidi wa kupumzika awe sawasawa, hata Yae Berko amekaa nje muda mrefu kwa sababu alipewa na siku za kupumzika,” alisema.Kuhusu wachezaji watakaokwenda Tanga, Sendeu alisema kwamba hadi sasa hawajaamua lakini watakuwa kati ya 20 na 25.Alisema hiyo inatokana na kwamba, wanasubiri Kikao cha Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kinachofanyika leo, ili waamue.Alisema hiyo inatokana na kwamba kikao hicho kinashikilia hatima ya wachezaji wao watano, waliositishiwa adhabu na Kamati hiyo iliyo chini ya Mwenyekiti Kamanda Mstaafu wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Alfred Tibaigana baada ya kufungiwa awali na kamati ya Ligi Kuu, hivyo kama watarejeshwa ‘rumande’ ina maana hawatakwenda Tanga.Kamati ya Tibaigana iliwaachia huru wachezji watano wa Yanga waliokuwa wamefungiwa kwa vipindi tofauti na Kamati ya Ligi ya TFF, baada ya kuridhika na utetezi wa klabu hiyo juu ya adhabu hizo.Akitangaza kusitisha adhabu hiyo, Tibaigana alisema kwa mujibu wa taratibu za TFF, Kamati ya Ligi haina mamlaka ya kumfungia mchezaji yeyote wala kutoa adhabu, isipokuwa Kamati ya Nidhamu.Kamati ya Ligi iliyokutana Machi 12, mwaka huu chini ya Mwenyekiti wake, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ iliwafungia wachezaji hao wa Yanga kwa tuhuma za utovu wa nidhamu walioufanya kwenye mechi ya Azam FC, Machi 10, mwaka huu, Uwanja wa Taifa.Mabeki Stefano Mwasika aliyempiga ngumi refa Israel Nkongo alifungiwa mwaka mmoja na faini ya Sh Milioni 1, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ alifungiwa mechi sita na faini ya Sh. 500,000, viungo Nurdin Bakari alifungiwa mechi tatu na faini Sh. 500,000 sawa na Omega Seme na mshambuliaji Jerry Tegete.Akiizungumzia mechi na Coastal Union, Sendeu alisema morali ni kubwa na wanaamini wanakwenda kuchukua pointi tatu huko.Alisema timu itaondoka mapema kesho na tayari mjini Tanga wamekwishaandaliwa mazingira ya sehemu salama ya kufikia, kufanya mazoezi na hata kula, ili kuhepa fitina za Wagosi ambao wamepania kweli kuiadhiri Yanga, kulipa kisasi cha 5-1 walizofungwa katika mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya Bara, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MATAJIRI YANGA WAMWAGA MAMILIONI MAZOEZINI COASTAL AFE JUMAMOSI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top