• HABARI MPYA

    Sunday, December 13, 2020

    KAPTENI BOCCO AFUNGA BAO PEKEE SIMBA SC YAWACHAPA MBEYA CITY 1-0 UWANJA WA SOKOINE

    Na Mwandishi Wetu, MBEYA
    MABINGWA watetezi, Simba SC wameibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.
    Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, Nahodha na mshambuliaji tegemeo wa timu, John Raphael Bocco dakika ya 32 akimalizia pasi ya kiungo Mzambia, Clotous Chama.
    Na kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 29 baada ya kucheza mechi 13 na kupanda hadi nafasi ya pili, sasa wakizidiwa pointi nane na vinara, Yanga SC ambao hata hivyo wamecheza mechi mbili zaidi.

    Mbeya City walimlalamikia refa Martin Saanya wa Morogoro aliyekuwa anasaidiwa na Mohamed Mkono wa Tanga na Frank Chavala wa Mwanza kukataa bao lao lililofungwa na chipukizi Dennis Kibu kipindi cha pili.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, mabao ya Adam Adam dakika ya 15 kwa penalti na Edward Songo dakika ya 17 yameipa JKT Tanzania ushindi wa 2-0 dhidi ya Biashara United Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.
    Nayo Coastal Union imelazimishwa sare ya bila kufungana na Tanzania Prisons Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.
    Kikosi cha Mbeya City kilikuwa; Lameck Kanyonga, Kenneth Kunambi, Mpoki Mwakinyuke, Juma Shemvuni, Babilas Chitembe, Edgar Mbembela, Daniel Lukandamila/Abdul Suleiman dk28, Suleiman Ibrahim/Rashid Mchelenga dk77, Kibu Denis/Abasarim Chidiebere dk87, Kelvin John na Richardson Ngondya.
    Simba SC; Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Ibrahim Ame, Joash Onyango, Jonas Mkude, Hassan Dilunga/Miraj Athumani ‘Madenge’ dk74, Said Ndemla/Erasto Nyoni dk81, Meddie Kagere, John Bocco/Chris Mugalu dk46 na Clatous Chama. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAPTENI BOCCO AFUNGA BAO PEKEE SIMBA SC YAWACHAPA MBEYA CITY 1-0 UWANJA WA SOKOINE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top