• HABARI MPYA

    Sunday, May 05, 2019

    NI DK MSOLLA NA MWAKALEBELA VIONGOZI WAPYA YANGA, TIBOROHA AAMBULIA KURA 60

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    ALIYEWAHI kuwa kocha Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Dk. Mshindo Mbette Msolla ndiye Mwenyekiti mpya wa klabu ya Yanga ya Dar es Salaam.
    Hiyo ni baada ya uchaguzi uliofanyika leo Bwalo la Maofisa wa Jeshi la Polisi, Osyterbay mjini Dar es Salaam akishinda kwa kishindo dhidi ya Dk. Jonas Benedict Tiboroha.
    Msolla amepata jumla ya 1,276 dhidi ya 60 tu za Daktari mwenzake, Tiboroha aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa klabu hiyo chini ya uongozi uliopita.
    Nafasi ya Makamu Mwenyekiti imekwenda kwa Katibu Mkuu wa zamani wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Frederick Mwakalebela aliyepata kura 1,206 akiwashinda Janneth Mbene (Mbunge)aliyepata kura 61, Titus Osoro kura 17, Yono Kevela kura 31 na Chota Chota kura 12.

    Dk. Mshindo Msolla (kushoto) akizungumza na Rais wa awamu ya Nne, Dk. Jakaya Kikwete wakati huo akiwa Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika

    Walioshinda nafasi za Ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Hamad Islam aliyepata 1,206, Mhandisi Bahati Faison Mwaseba kura 1,174, Dominick Ikute kura 1,088, Kamugisha Kalokola kura 1,072, Arafat Haji kura 1,024, Salum Ruvila kura 976, Saad Khimji kura 788 na Rodgers Gumbo kura 776. 
    Uchaguzi huu umefuatia kujiuzulu kwa viongozi wote waliongia madarakani Juni 11 mwaka 2016, Mwenyekiti Yussuf Manji, Makamu Mwenyekiti, Clement Sanga na wajumbe wao, Siza Augustino Lymo, Tobias Lingalangala, Samuel Lukumay, Hussein Nyika, Omary Said Amir, Salum Mkemi, Ayoub Nyenzi na Inspekta Hashim Abdallah.
    Pamoja na kuwa kocha wa Taifa Stars, Dk. Msolla pia amewahi kuwa mtumishi wa Serikali kwa nafasi mbalimbali, ikiwemo Ukurugenzi wa Uendelezaji wa Mazao katika Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika wakati wa awamu ya Nne chini ya Rais Dk. Jakaya Mrisho Kikwete.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI DK MSOLLA NA MWAKALEBELA VIONGOZI WAPYA YANGA, TIBOROHA AAMBULIA KURA 60 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top